Monday 15 July 2013

Twiga Bancorp yatua Bunda


Na Ahmed Makongo
WAFANYABIASHARA na Kandarasi wanaofanya kazi na halmashauri ya wilaya ya Bunda, wametakiwa kufungua akaunti katika benki zilizopo wilayani humo, ili kusaidia kuinua uchumi.
Mkuu wa Wilaya ya Bunda Joshua Tuppa, alitoa wito huo juzi, alipokuwa akifungua kituo cha kutolea huduma za kibenki cha Twiga Bancorp.
Mirumbe, alisema wilaya hiyo ni ya uwekezaji wa kibiashara. Vyema wale wote wanaopatiwa zabuni katika halmashauri hiyo, wakafungua akaunti katika benki hizo.
Alisema kuanzia sasa kandarasi yeyote anayeomba kazi katika halmashauri hiyo, lazima awe ana akaunti kwenye benki iliyoko wilayani humo, kinyume na hapo, hawatapatiwa zabuni.
Mkuu huyo wa Wilaya, alizitaja benki hizo kuwa ni Twiga Bancorp, inayomilikiwa na serikali kwa asilimia 100 na NMB.
“Tutafanya utaratibu ili mkandarasi anayefunga mkataba na halmashauri yetu lazima awe na akaunti ya Benki yoyote iliyoko wilayani kwetu…Unajua hali hiyo itafanya mzunguko wa pesa kuwa mkubwa na uchumi wa wilaya yetu utakuwa” alisema.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Twiga Bancorp Limited, Profesa Ammon Mbelle, alisema benki hiyo ndiyo pekee  nchini inayomilikiwa na serikali kwa aslimia 100.
Alisema ni vyema kwa kila Mtanzania popote  alipo, aitumie ipasavyo.
Profesa Mbelle, alisema dhana ya benki hiyo ni kuungana na umma wa Watanzania waliodhamiria kuboresha hali ya maisha yao pamoja na kulijenga taifa kiuchumi.
 Naye Mkuu wa Shughuli za Utendaji wa Kibenki wa benki hiyo, Richard Kambole, alisema kituo hicho cha Bunda ni cha kwanza kufunguliwa nchini na wilaya hiyo imepewa kipaumbele.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru