Wednesday 24 July 2013

Masele: Wakamateni watoroshaji madini


Na Mohammed Issa
WAKALA wa Ukaguzi wa Madini Tanzania (TMAA), wametakiwa kuwadhibiti na kuwakamata wale wote wanaotorosha madini nje kwa njia za panya.
Hatua hiyo imetajwa kuwa itasaidia kuokoa rasilimaliza za taifa, ambazo zipo kwa ajili ya kuwanufaisha Watanzania.
Agizo hilo lilitolewa jana na Naibu Waziri wa Nishati na Madini anayeshughulikia Madini Stephen Masele, alipozungumza na Baraza la Wafanyakazi la wakala huo.
Alisema baadhi ya wafanyabiashara wanadaiwa kutorosha madini nje na kwamba, TMAA inapaswa kuendelea kuwabana zaidi ili kuokoa rasilimali hiyo.
Naibu Waziri huyo, alisema TMAA inafanya kazi kubwa na nzuri, hivyo, haina budi kuongeza kasi ili kuleta tija kwa Watanzania kwa kuokoa rasilimali zinazotaka kutoroshwa.
Pia, alitumia fursa hiyo kuwataka kuendelea kuwabana wachimbaji wadogo kwa kuhakikisha wanalipa kodi stahiki za serikali.
“Nawapongezeni kwa kazi nzuri mnayoendelea kuifanya, lakini ongezeni juhudi zaidi, wale wote wanaojaribu kutorosha rasilimali za taifa wadhibitiwe. “Wakamateni wote watakaobainika kutorosha madini,” alisema Masele na kuongeza: Madini ni miongoni mwa rasilimali muhimu za taifa, lazima zipate usimamizi na ulinzi wa kutosha.
Kuhusu wachimbaji wadogo wa madini kubanwa, Masele alisema baadhi hufanya ujanja kwa kukwepa kulipa kodi hivyo kupoteza mapato ya serikali.
Kwa mujibu wa Masele, kiasi kikubwa cha fedha za serikali hupotea kutokana na wachimbaji wadogo kukwepa kodi.
Naye Mtendaji Mkuu wa TMAA Mhandisi Paulo Masanja, alisema wakala huo umepata mafanikio makubwa tangu kuanzishwa kwake.
Alisema hivi sasa wanazidi kusonga mbele katika kutekeleza wajibu waliopewa na serikali.
Mhandisi Masanja, alisema baadhi ya wamiliki wa migodi mikubwa na midogo, wameanza kulipa kodi stahiki za serikali na kiasi cha sh. bilioni 473.9 kimekusanywa toka 2009 mpaka sasa.
Alisema kutokana na kuimarisha kwa ukaguzi wa kimkakati unaofanywa na TMAA, zaidi ya sh. bilioni 1.8 zimekusanywa kwa wachimbaji wa madini ya ujenzi katika mikoa ya Dar es Salaam na Pwani, zikiwa ni mrahaba.

MTENDAJI Mkuu wa Wakala wa Madini Tanzania (TMAA), Mhandisi Paulo Masanja akizungumza na Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi la Wakala huo, lililoketi jijini Dar es Salaam, jana. Anayefuata ni Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Stephen Masele.
WAJUMBE wa Baraza la Wafanyakazi la Wakala wa Madini Tanzania (TMAA) wakiwa katika picha ya pamoja na Naibu Waziri Masele baada ya kufungua kikao cha Baraza hilo kilichofanyika jana katika Hoteli ya Giraffe jijini Dar es Salaam.
MJUMBE wa Baraza la Wafanyakazi la Wakala wa Madini Tanzania (TMAA), akitoa mada kwenye mkutano wa baraza hilo uliofanyika jana mjini Dar es Salaam.
WAJUMBE wa Baraza la wafanyakazi la WAkala wa Madini Tanzania (TMAA) wakiwa kwenye kikao cha baraza hilo kilichofanyika jana Dr es Salaam.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru