Friday 19 July 2013

Miili ya askari JWTZ kuletwa leo


Na Mwandishi Wetu
MIILI ya askari saba wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), waliouawa Darfur, nchini Sudan, inawasili leo alasiri.
Askari hao waliuawa wiki iliyopita, baada ya kushambuliwa na waasi katika jimbo hilo. Wengine 14 walijeruhiwa.
Miili ya askari hao itawasili kwa ndege maalumu ya Umoja wa Mataifa, katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es Salaam, saa tisa alasiri.
Taarifa iliyotolewa jana, mjini  Dar es Salaam, kwa vyombo vya habari na Kurugenzi ya Habari na Uhusiano, Makao Makuu ya Jeshi ilisema baada ya kuwasili miili hiyo itapelekwa Hospitali ya Rufani ya Jeshi ya Lugalo.
Imeelezwa miili hiyo itaagwa keshokutwa, saa tatu asubuhi, katika viwanja vya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Upanga, Dar es Salaam.
Taarifa hiyo ilisema miili ya askari hao itaagwa kwa heshima za kijeshi na baadaye itakabidhiwa kwa ndugu kwa ajili ya maziko.
Hadi sasa waasi waliohusika na shambulio hilo hawajakamatwa, ambapo Rais Jakaya Kikwete, akizungumza na Rais Omar al Bashir wa Sudan, alimtaka kuchukua hatua za haraka kuwasaka na kuwakamata waliohusika na mauaji ya askari hao.
Rais al Bashir aliyezungumza na Rais Kikwete kwa njia ya simu, alisema anaamini waliohusika ni wahalifu, hivyo watasakwa na kuchukuliwa hatua.
Umoja wa Mataifa umeahidi kuzilipa fidia familia za askari hao kiasi cha sh. milioni 100 kila moja.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru