Tuesday 16 July 2013

Babu amuua mjukuu kwa kumchapa bakora


NA ANITA BOMA , NJOMBE
MTOTO mwenye umri wa miaka miwili, Gift Fute, amekufa baada ya kupigwa fimbo na babu yake kwa madai ya kukutwa akichezea maji na wenzake.
Gift ambaye ni mkazi wa Kijiji cha Ikwega, Wilaya ya Wanging’ombe, mkoani hapa, alikutwa na mkasa huo, Julai 13, mwaka huu, saa moja jioni.
Kamanda wa Polisi mkoani hapa Fulgence Ngonyani, jana alisema mtoto huyo alikuwa akichezea maji na wenzake ndipo babu yake Nicolaus Fute (78), aliamua kumchapa na fimbo kwa lengo la kumwadhibu.
Alisema marehemu baada ya kuchapwa, inadaiwa aliumia na alipelekwa katika zahanati ya Usuka kwa matibabu, lakini alikufa akiwa anaendelea kutibiwa.
Kamanda Ngonyani, alisema chanzo cha tukio hilo ni kipigo kilichotoka kwa mtuhumiwa huyo ambaye alikamatwa kuhusiana na tukio hilo.
Wakati huohuo;  mkazi wa Kijiji cha Lyamluki mkoani hapa, Hilda Mtega (86), amekutwa amekufa ndani ya nyumba yake.
Kamanda Ngonyani alisema tukio hilo lilitokea Julai 14, mwaka huu, saa tano asubuhi.
Alidai kuwa marehemu alikuwa na tabia ya kwenda kanisani kushiriki Ibada na mambo mengine ya kidini, baada ya kutoonekana kwa siku kadhaa, ndipo waumini wenzake waliamua kwenda nyumbani kwake kujua kulikoni na ndipo walipobaini kuwa amekufa.
Aidha, Kamanda huyo alisema chanzo cha tukio hilo hakijajulikana ingawa inadaiwa huenda marehemu amekufa kutokana na shinikizo la damu, alikuwa akiishi peke yake.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru