Friday 27 June 2014

CCM yalia na watumishi wahujumu



Na Ahmed Makongo, Bunda
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) mkoani Mara, kimesema baadhi ya watumishi wa serikali mkoani humo, wanaihujumu serikali pamoja na ilani ya uchaguzi ya Chama.
Katika madai yake hayo, CCM imesema watumishi hao wanafanya hivyo kwa kutokuwajibika ipasavyo katika kutekeleza majukumu yao ikiwa pamoja na kusimamia kikamilifu utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mara, Christopher Sanya, alitoa shutuma hizo kwa nyakati na maeneo tofauti, wakati akihutubia vikao vya ndani na kwenye mikutano ya hadhara kwenye tarafa za Kenkombyo, Nansimo na Chamriho.
Sanya alisema baadhi ya watumishi wa serikali wanaihujumu serikali na ilani ya Chama, kwa kushindwa kusimamia utekelezaji wa ilani hiyo ipasavyo. Alsiema  hali hiyo imekuwa ikisababisha baadhi ya miradi ya maendeleo kuwa chini ya kiwango na kutokukamilika kwa wakati, hivyo wananchi kuichukia serikali yao.

 “Hapa tunagundua kwamba ni kweli baadhi ya watumishi wa serikali ndio wanaoihujumu serikali na Chama chetu na wanafanya makusudi kabisa kutuharibia. Kama Chama tunasema hatutaki mambo hayo yaendelee kuwepo, wanatupatia wakati mugumu sana kukinadi Chama kwa wananchi,” alisema.

Alisema  baadhi ya watumishi hao wanaihujumu pia serikali ya CCM  kwa kutokutoa huduma zinazostahili kwa jamii hasa  katika sekta za afya, maji, elimu na miundombinu.
Akitoa mfano katika sekta ya afya, alisema baadhi ya waganga na wauguzi wamekuwa wakiuzia wajawazito na watoto kadi za kliniki ambazo hutolewa bure na serikali, hali ambayo inaichafua serikali ya CCm.
Alisema katika sekta ya ujenzi baadhi ya watumishi wa serikali wamekuwa wakishirikiana na wakandarasi kuhujumu miradi inayotekelezwa na hivyo kujinufaisha na fedha za miradi hiyo, kinyue cha sharia.
Aliongeza kuwa hali hiyo imekuwa ikikichafua chama hicho, kwani ndicho chenye serikali na kwamba CCM mkoani Mara, haitavumilia hali hiyo iendelee kuwepo kwa sababu fedha zinazotolewa kwenye miradi hiyo zinatokana na kodi ya wananchi.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru