Monday 16 June 2014

‘Teueni wanaokubalika’


NA LATIFA GANZEL, MOROGORO
VIONGOZI na wanachama wa CCM wameshauriwa kujenga tabia ya kumteua kiongozi anayekubalika na wananchi na sio kumchagua kiongozi kwa sababu anapendwa na viongozi wa juu au anatoa rushwa.
Ushauri huo ulitolewa na Meya wa Manispaa ya Morogoro,  Amir Nondo alipokuwa akifungua semina ya makatibu wa CCM kutoka Manzese jijini Dar es Salaam na wenyeji wao kutoka Kata ya Boma mkoani hapa.
Nondo alisema katika kuelekea uchaguzi wa watendaji wa serikali za mitaa Oktoba, mwaka huu, ni vyema wakafanya utafiti mapema na kuweka akili zao katika hilo ili kuweza kufahamu nani anafaa kuwa kiongozi na anayependwa na wananchi katika mitaa yao.
Naye, Katibu Kata wa CCM,  Kata ya Manzese, Ramadhani Kidoga, alisema lengo la semina hiyo ni kutoa elimu kwa kujiandaa na uchaguzi wa serikali za mitaa Oktoba, mwaka huu.
Alisema waliamua kuwalenga makatibu kwa kuwa ndiyo wakurugenzi, watendaji wakuu na pia ndiyo muhimili mkuu ndani ya Chama.
Pia, alisema anaamini wakitoka katika semina hiyo, makatibu hao watakuwa viongozi wenye weledi na mfano wa kuigwa kwa viongozi wengine.
Pia, alisema wanaamini siku zote ni ushindi katika CCM, lakini ni vyema wakajipanga kwa ajili ya uchaguzi mkuu.
Baada ya kumaliza semina hiyo, viongozi hao walifanya ziara  katika Hifadhi ya Mikumi kwa ajili ya kufanya utalii wa ndani.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru