Tuesday 3 June 2014

Vigogo Manispaa Kinondoni waendelea kusota rumande


NA MWANDISHI WETU
VIGOGO watatu wa Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni, waliokamatwa kwa tuhuma za kuomba na kupokea rushwa, wanaendelea kushikiliwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).
Vigogo wanaoshikiliwa ni Mhandisi wa manispaa hiyo, Baraka Mkuya, Mkaguzi Mkuu wa Majengo aliyetajwa kwa jina moja la Christopher na Ofisa Mtendaji wa Kata ya Msasani aliyefahamika kwa jina la Mushi.
Ofisa Uhusiano wa TAKUKURU, Doreen Kapwani, alisema jana jijini Dar es Salaam kuwa vigogo hao wanaendelea kuwashikilia kwa ajili ya uchunguzi zaidi.
Mhandisi Mkuya na wenzake walikamatwa mwishoni mwa wiki kwa madai ya kuomba na kupokea rushwa na kwa mujibu wa Doreen, wanatarajiwa kufikishwa mahakamani baada ya uchunguzi kukamilika.
Habari za uhakika zilizolifikia gazeti hili kutoka katika manispaa hiyo zilidai kuwa,  vigogo hao wanatuhumiwa kutoa kibali cha kuweka mabango ya matangazo kwa kampuni iliyotajwa kwa jina la Masoko bila kufuata utaratibu.
Inadaiwa kuwa mabango hayo ya matangazo yamewekwa katika  maeneo ya Oysterbay katika barabara inayotoka Coco Beach kwenda Masaki, wilayani Kinondoni, Dar es Salaam.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru