Monday 30 June 2014

Vikwazo vya kibiashara dhidi ya Czech kuondolewa


NA SUBIRA SAID, TSJ
SERIKALI imeandaa mpango wa kuondoa vikwazo vinavyokwamisha ukuaji wa biashara na Jamhuri ya Czech.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji na Uwezeshaji), Dk. Mary Nagu, alisema hayo jana alipokuwa akifungua kongamano la kibiashara kati ya Tanzania na Jamhuri ya Czech.
Alisema mpango huo utawawezesha wawekezaji na wafanyabiashara kutumia fursa zilizopo ili kukuza uchumi na maendeleo ya nchi hizo.
Dk. Mary alisema tayari serikali imetayarisha mpango huo na inatarajia kuupeleka Czech ili iweze kuainisha vikwazo vilivyopo.
“Mpango huo ukikamilika tuna imani tutaweza kuondoa vikwazo vilivyopo na kuonyesha maeneo mbalimbali ya ushirikiano wa kibiashara,” alisema.
Alisema maendeleo katika sekta ya uwekezaji hayawezi kufikiwa bila ya kuondoa vikwazo vya utozwaji kodi mara mbili pamoja na ukiritimba.
Kwa upande wake, mwakilishi kutoka serikali ya Czech, Pavel Rezac, alisema kongamano hilo litasaidia kukuza na kutambua fursa mbalimbali za biashara na uwekezaji.
Kongamano hilo ni la kwanza kufanyika nchini na linawashirikisha wadau mbalimbali wa kibiashara kutoka ndani na nje ya nchi.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru