Monday 30 June 2014

Serikali yatakiwa kusimamia gesi kwa maendeleo ya taifa


NA MWANDISHI WETU
SERIKALI imeshauriwa kuwekeza mapato ya rasilimali zake hususan mafuta na gesi ili kuleta maendeleo endelevu kwa manufaa ya kizazi cha sasa na baadaye.
Vile vile imetakiwa kuhaikisha matumizi ya ndani kwenda sambamba  na mapato hayo ikiwemo kuongeza tija katika matumizi ya sekta za umma katika ngazi zote.   
Mkurugenzi wa kampuni ya Pan African Energy, Patrick Rutabanzibwa, alisema hayo jijini Dar es Salaam jana kwenye mkutano wa kujadili mikakati ya kuhakikisha rasilimali zilizopo zinawanufaisha wananchi ulioandaliwa na Taasisi ya Uongozi.
Rutabanzibwa, ambaye amewahi kuwa Katibu Mkuu katika wizara kadhaa ikiwemo ya Nishati na Madini, alikuwa mwezeshaji wa mkutano huo ulioshirikisha nchi washirika wa maendeleo. 
Alisema ni muhimu serikali ikazingatia mapendekezo hayo kwani ipo siku raslimali hizo zitakwisha.
“Miongoni mwa mambo ya msingi yaliyojadiliwa ni umuhimu wa serikali kuweka wazi mikataba itakayoingia na kampuni mbalimbali katika sekta hiyo pamoja na kuhakikisha inapata mgawanyo mkubwa wa asilimia na wa haki ili utumike kuleta tija katika maendeleo ya taifa,” alisema.
Alisema jambo lingine la msingi lililojadiliwa ni kuwepo kwa uwazi wa mikataba hiyo kutoka mamlaka zinazohusika ili wananchi waweze kusimamia raslimali za nchi yao.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru