Monday 30 June 2014

HELSB yatangaza kiama kwa waajiri


NA MWANDISHI WETU
BODI ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HELSB), imewatangazia kiama waajiri watakaoshindwa kuwasilisha taarifa za watumishi waliokopa katika bodi hiyo.
Imesema haitakuwa na huruma na waajiri hao na kwamba itawafikisha mahakamani.
Mkurugenzi Msaidizi Urejeshaji Mikopo wa HELSB, Robert Kibona, alisema hayo jana mjini Dodoma katika kutano mkuu wa mwaka wa wakurugenzi wa Utawala na Raslimali watu serikalini.
Alisema tayari waajiri watano wamechukuliwa hatua kutokana na kushindwa kuwasilisha taarifa za watumishi wanaodaiwa na bodi hiyo.
Kibona alisema mwajiri atakayeshindwa kutoa taarifa za wahitimu wa elimu ya juu kwenye bodi kwa wakati, atatakiwa kulipa faini ya sh. milioni saba au kutumikia kifungo kisichopungua miezi 12  jela au vyote kwa pamoja.
Alisema hadi sasa waajiriwa 18 wamefikishwa mahakamani kwa kosa la kushindwa kurejesha mikopo hiyo.
Kibona alisema ili kufanikisha kazi ya urejeshaji  mikopo kutoka kwa wadaiwa,  HELSB iko mbioni kutunga  sheria na mifumo  mbalimbali ya kuwadhibiti wadaiwa hao.
ìTunatarajia sheria ambazo zitawazuia wadaiwa wa mikopo ya elimu ya juu kupata hati ya kusafiria nje ya nchi au kibali cha kusafiri hadi atakapowasiliana na bodi,” alisema.
Alisema mhitimu atakayeshindwa kulipa mkopo, taarifa zake zitatangazwa kwenye vyombo vya habari na kwenye taasisi za mikopo ili asipate huduma yoyote ya kifedha.
Naye, Msaidizi wa Mtendaji Mkuu Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu, Veronica Nyahende, aliwataka wahitimu wa elimu ya juu nchini kutumia elimu waliyonayo kujiajiri,  badala ya kusubiri kuajiriwa.
Alisema changamoto ya kurejesha mikopo  ni kubwa kwa upande wa wahitimu wa elimu ya juu ambao hawana kazi ama hawajajiajiri.
Veronica alisema Bodi imeingia mkataba na kampuni itakazokusanya mikopo kwa walionufaika lakini wakashinda kuirudisha.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru