Friday 27 June 2014

‘Wabeshi’ waleta balaa mgodini



Na Chibura Makorongo, Shinyanga
SERIKALI imeombwa kulipatia ufumbuzi tatizo la vijana wanaojiita “wabeshi” wanaovamia mgodi wa almasi wa Williamson Diamonds Ltd ulioko Mwadui, Kishapu mkoani hapa.
Vijana hao wamekuwa wakivamia mgodi huo kwa lengo la kupora mchanga wa almasi na kujikuta wakipoteza maisha au kupata vilema vya maisha.
Ombi hilo lilitolewa  hivi karibuni na wakazi wa vijiji vinavyozunguka mgodi wa Almasi wa Mwadui ambapo walisema kwa kipindi kirefu vijana wengi wanaovamia mgodi huo wanapoteza  maisha .
Wakazi hao walisema imefika wakati sasa kwa serikali kufanya utafiti ili kuweza kuwabaini watu wanaowafadhili vijana hao kwa kuwapatia fedha kidogo na vitendea kwa kazi kwa ajili kufanya uvamizi kwa makubaliano ya kuwauzia almasi watakazozipata.
Mkazi wa kijiji cha Masagala, Hubi Mlyandengu, aliiomba serikali iwachunguze baadhi ya polisi ambao wanatuhumiwa kupokea fedha kutoka kwa makundi ya wabeshi na kuruhusu vijana hao kuingia mgodini kwa lengo la kupora mchanga wenye madini ya almasi.
Alisema vijana hao ni sawa bomu linalosubiri kulipuka kwani kuna hatari kutokea mapigano makubwa kati yao na walinzi wa mgodi, alitoa mfano wa tukio la wiki iliyopita kundi la wabeshi likiwa na silaha za jadi lilipovamia mgodini na kusababisha kifo cha mtu mmoja.
Hata hivyo, habari za kuaminika tayari serikali imeanza mikakati ya kuwadhibiti vijana hao na watu wanaowatuma na kwamba, operesheni hiyo imekuwa ikifanyika kimya kimya ili kuhakikisha wengi zaidi wanatiwa mbaroni.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru