Tuesday 14 April 2015

Serikali yamaliza mgogoro Hifadhi ya Saadani


NA CHRISTOPHER LISSA
HATIMAYE serikali imeumaliza  rasmi mgogoro wa ardhi  uliodumu kwa kipindi kirefu  baina ya Wizara ya Maliasiali na Utalii  na Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, unaohusisha eneo Hifadhi ya  Taifa ya Saadani.
Aidha  serikali  imeiagiza Halmashauri  ya Wilaya ya Bagamoyo , kukaa na Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA)  na wadau,  kurejea  mipaka ya zamani  ya eneo hilo, ili kuepusha mgongano usio na tija.
Mgogoro huo uliibuka mwaka  mwaka 2005,  baada ya serikali kuipandisha hadhi mbuga ya wanyama pori ya Saadani kuwa  Hifadhi ya Taifa na kumpa mwekezaji.
Alisema  eneo hilo lilitolewa  kwa  mtu aliyefahamika  kwa jina la Lazaba, kutoka Zanzibar, kwa ajili ya shughuli za  kunenepeshea mifugo,  ambapo wananchi walilalamikia  kuwa mipaka  mipya ya hifadhi hiyo iliingia katika  eneo lao, hali iliyoibua mgogoro mkubwa baina yao, TANAPA  na mwekezaji.
Tamko hilo  la kumaliza  mgogoro huo limetolewa hivi karibuni na Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, ambaye alitembelea eneo la mgogoro pamoja na Hifadhi ya Taifa ya Saadani, akiwa na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo  Dk. Adelhelm Meru, pamoja na viongozi mbalimbali wa Wilaya ya Bagamoyo na TANAPA.
Nyalandu alisema kuwa  ameamua kumaliza rasmi mgogoro huo,  baada  ya kuridhishwa na taarifa  aliyopewa na Katibu Mkuu wake Dk. Meru,  Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Abdulkadir Lamiya na  Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Shukuru Mbato.
Alisema kuwa  mgogoro huo hauna tija kwa maendeleo ya taifa,  kwani dhima ya wizara yake ni kuona  maeneo yote tengefu, zikiwemo mbuga za wanyama, vivutio mbalimbali, mapori ya akiba na hifadhi za taifa  yanakuwa ni maeneo rafiki kwa watu wanaoishi jirani.
“ Serikali italinda  kwa nguvu zote maeneo hayo  ili kutunza raslimali  pamoja na mipaka iliyowekwa. Ni marufu kuachia maeneo hayo muhimu.
Itakuwa siyo busara  kuendeleza migogoro isiyo na tija kama huu wa  Bagamoyo, ambao haukuwa na ulazima wa kuwepo.
Hakuna haja ya wananchi wanaoishi karibu na hifadhi zetu kuishi kwa mashaka na kujenga uhasama na wawekezaji au walinzi wetu wa maeneo haya,” alisema Nyalandu.
Aliongeza: “Nikiwa  waziri  mwenye dhamana,  ninatamka kuwa mgogoro huu  umemalizwa rasmi  na ninaagiza  TANAPA na Halamshauri ya Wilaya ya Bagamoyo kurejea upya  mipaka   iliyokuwepo awali kwa mujibu wa sheria. Pia ninaagiza GN namba 281 ya mwaka 2005,  ifanyiwe marekebisho  haraka  na kuiwasilisha kwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania,  ili kuhakikisha kuwa mgogoro huu unamalizika kabisa.”
Nyalandu aliagiza kuwa eneo la mgogoro la Lazaba,  wananchi wapange  matumizi  endelevu  kwa kuzingatia   zaidi kwamba eneo hilo liko karibu na Hifadhi ya Taifa ya Saadani.
Awali, Katibu Mkuu alimweleza  Nyalandu kuwa  mgogoro wa eneo la Lazaba ulidumu kwa  muda mrefu  na kusababisha  shughuli za maendeleo katika eneo hilo kusimama.
“Wawekezaji wanashindwa  kufanya shughuli za maendeleo katika eneo hili. Pia  wananchi wanaogopa  kuingia   katika eneo la hilo na kuyaendeleza maeneo yao.
Akieleza historia  fupi  ya mgogoro huo, Mwenyekiti wa Halmshauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Mbato, alisema kuwa   mwaka 1976, eneo hilo lilitolewa kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), kwaajili ya  kutumika kama eneo la kunenepeshea mifugo.
“Hata hivyo, wakati   serikali ikiipandisha hadhi mbuga ya wanyama  pori ya Saadani kuwa Hifadhi ya Taifa, wakati wanapima mipaka,  ilionekana sehemu  hiyo ya mgogoro  imeingia kwenye eneo la  wananchi,  hivyo kuibua mgogoro mkubwa baina ya TANAPA na wananchi wa eneo hilo,  pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru