Tuesday 14 April 2015

Wanaswa na meno ya tembo


NA LATIFA GANZEL, MOROGORO
WATU watano wanashikiliwa na polisi kwa tuhuma  ya  kukutwa na vipande vinane  vya  meno  ya  tembo, vikiwa vimevificha kwenye dumu la  mafuta.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Leonard Paul, alisema tukio  hilo lilitokea jana, saa 2:30 usiku katika eneo  la  Daraja Mbili, barabara  ya  kwenda Mikumi wilayani Kilosa.
Alisema watuhumiwa hao walikamatwa na polisi kwa kushirikiana na askari wa  wanyamapori, waliokuwa kwenye  doria.
Paul alisema  watu  hao walichukua  dumu  la  lita  20 la mafuta na  kulipasua  na  kwamba ndani  yake waliingiza vipande vya meno ya tembo na kuvipakia  kwenye gari la mizigo aina  ya  Mitsubishi Fuso   lenye namba  za  usajili T 770 ABG.
Alisema   gari hilo lilikuwa limepakia shehena ya pumba na kreti za soda, ambapo dumu hilo liliwekwa  katikati.
Paul aliwataja  watuhumiwa hao kuwa ni Mohamed Juma (48) mkazi wa Mtawala  Morogoro, Juma  Athuman (35) mkazi wa Kiberege na Said  Salum (23) ambaye ni utingo wa  Fuso na mkazi wa Morogoro.
Wengine ni Omary Marumbo (26) mkazi wa Morogoro  na Victoria Festo (43), ambaye ni mfanyabiashara na mwenye mzigo wa  pumba  iliyokuwa kwenye  gari  hilo.
Alisema watuhumiwa wanatarajiwa  kufikishwa mahakamani wakati wowote baada ya upelelezi kukamilika.


Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru