Tuesday 7 April 2015

Ushirikiano Bara na Zanzibar kudumu



NA MWANDISHI WETU, ZANZIBAR
MJUMBE wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM, Balozi Seif Ali Iddi, amesema Watanzania wanaoishi Zanzibar na Bara, wataendelea kushirikiana kwa miaka mingi zaidi kutokana na mwingiliano wao wa kidamu.
Balozi Seif Ali Iddi
Alisema uwepo wa ushirikiano huo ndio njia pekee itakayotoa fursa kwa Watanzania hao kusaidiana katika kutatua changamoto zinazowakabili miongoni mwao na vizazi vyao.
Balozi Iddi ambaye pia ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, alisema hayo wakati akizungumza katika mkutano wa ujirani mwema kati ya wanachama  wa CCM na viongozi wa Mkoa wa Magharibi, Unguja  na kutoka  Kata ya Mtoni, Wilaya ya Temeke, Dar es salaam.
Mkutano huo ulifanyika katika Tawi la CCM, Mwanakwerekwe B, kufuatia ziara za ujirani mwema kati ya pande hizo mbili.
Balozi Iddi alisema hakuna kikundi wala mtu anayeweza kuung’oa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, kutokana na historia yake kwa jinsi ulivyoimarika  kwa miaka kadhaa iliyopita.
Katika hatua nyingine,  Balozi Iddi aliwataka na kuwaomba Watanzania wote kuiunga mkono katiba inayopendekezwa.
Balozi Iddi alisema katiba inayopendekezwa ina muundo wa mfumo waserikali mbili, ambazo zitadumisha muungano kwa miaka 50 ijayo.
Akizungumzia suala la uchaguzi mkuu  unaotarajiwa kufanyika  Oktoba, mwaka huu, Balozi Iddi aliwataka wanachama wa CCM, kuheshimu maamuzi ya vikao vya chama wakati wa kuteua wagombea.
Alisema ni vyema kwa wanachama kukubali maamuzi yanayotolewa na chama kwa kuwaunga mkono wagombea waliopendekezwa katika ngazi zote.
Katibu wa kamati ya ujirani mwema, Muhidini Makame Ussi, alisema ujirani mwema kati ya Kata ya Mtoni na Wilaya ya Dimani, ulianza mwaka 1995.
Ussi alisema ujirani mwema huo unaojumuisha viongozi na wanachama wa chama wa pande hizo mbili.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru