Tuesday 4 March 2014

MBIO ZA UBUNGE CHALINZE


Ridhiwani, Madega  na Maneno vitani

  • Wachukua fomu kumrithi Bwanamdogo
  • Mchuano kura za maoni kutikisa Msata

NA MWAMVUA MWINYI, BAGAMOYO

HARAKATI za kuwania ubunge katika Jimbo la Chalinze, mkoani Pwani,  zimezidi kushika kasi ambapo makada maarufu wa CCM, wamechukua fomu kuwania kuteuliwa.
Uchaguzi huo unafanyika kutokana na kifo cha aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Saidi Bwanamdogo, aliyewatumikia wananchi kwa kipindi cha miaka mitatu.

Ridhiwani Kikwete
Mnyukano wa kuwania kuteuliwa na CCM kuwania nafasi hiyo unatarajiwa kuwa mkali kutokana na nguvu walioyo nayo makada waliochukua fomu ambao ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM kutoka  Wilaya ya Bagamoyo, Ridhiwani Kikwete, na aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa Klabu ya Yanga, Iman Madega.
Wengine ni Mkuu wa Wilaya ya Kigoma, Ramadhan Maneno, ambaye pia alikuwa kuwa mbunge wa jimbo hilo kabla ya kuangushwa kwenye kura za maoni na Bwanamdogo.
Pia kwenye mpambano huo wamo Waziri Omari Kabanga na Changwa Mohamed, ambaye ni mwanamke pekee.
Katibu wa CCM Mkoa wa Pwani, Sauda Mpambalyoto, alisema fomu zilianza kutolewa Ijumaa iliyopita na kwamba mwisho wa kurejesha kwa wagombea wote ilikuwa jana.
Alisema kati ya wagombea watano waliochukua fomu ni Kabanga pekee ambaye hakurejesha na kwamba, kinachosubiriwa ni taratibu zingine za Chama.
‘’Uchukuaji fomu ulikwenda vizuri na wagombea wote waliafuata taratibu, wanne wamerudhisha fomu lakini Kabanga hakuweza kutimiza masharti kwa maana hakurejesha fomu zake. Tunasubiri tataribu zaidi ili wagombea washiriki kwenye kura za maoni na baadaye vikao vya juu kutoa maamuzi ya uteuzi,’’ alisema Sauda.
Aliongeza kuwa mkutano kwa ajili ya wanachama kuwapigia kura za maoni wagombea hao utafanyika leo katika Kata ya Msata na baadaye matokeo yatapelekwa kwenye vikao vya juu.
Tayari Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), imetangaza ratiba ya uchaguzi huo ambao Machi 12, mwaka huu. Uteuzi wa wagombea utafanyika kisha kufuatiwa na kampeni zitakazoanza Machi 13, mwaka huu na Aprili 6, itakuwa siku ya kupiga kura.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru