Wednesday 19 March 2014

Rais Kikwete kunguruma kesho


NA MAGRETH KINABO, DODOMA
RAIS Jakaya Kikwete, kesho atalihutubia Bunge Maalumu la Katiba mjini hapa.

Katibu wa Bunge, Yahya Khamis Hamad, alisema hayo jana, alipozungumza na waandishi wa habari na kwamba, Rais Kikwete atahutubia kwa wa saa moja.
Alisema kwa mujibu wa kanuni za bunge, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania atalihutubia Bunge Maalumu saa 10 jioni.
Yahya alisema ratiba ya shughuli hiyo itaanza na kikao cha Bunge saa 9.10 alasiri.
Baada ya kuwasili viwanja vya Bunge, alisema Rais Kikwete atapokewa na viongozi wa bunge ambao ni Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti, Katibu na Naibu Katibu.
Alisema Rais atakwenda jukwaa maalumu kupokea salamu za heshima na kukagua gwaride lililoandaliwa na Jeshi la Polisi.
Katibu alisema viongozi wataingia bungeni kwa maandamano ambao ni
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi, Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Sheni, Rais Kikwete, atakayefuatana na Mwenyekiti wa Bunge, Samuel Sitta.
Yahya alisema viongozi wengine walioalikwa ni wa kitaifa na watendaji wakuu kutoka pande zote za Muungano; marais, mawaziri wakuu, waziri kiongozi na maspika wastaafu.
Pia wajane wa waasisi wa Muungano, mama Maria Nyerere na Fatuma Karume; Mwenyekiti na wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Wengine ni wawakilishi kutoka taasisi za dini, zisizo za kiserikali, tasnia ya habari, vyama vyote vya siasa vyenye usajili wa kudumu, taasisi za elimu, vyama vya watu wenye ulemavu na wafanyakazi, wafugaji, wavuvi, wakulima na kutoka sekta binafsi.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru