Monday 15 July 2013

Aliyemjeruhi sheikh kwa tindikali mbaroni


NA LILIAN JOEL, ARUSHA
POLISI inamshikilia Mustafa Kiduka (50), kwa tuhuma za kummwagia maji yanayodaiwa tindikali Kaimu Sheikh wa wilaya ya Arumeru, Said Makamba, na kumsababisha maumivu makali usoni na kifuani.
Sheikh Makamba alimwagiwa maji hayo Ijumaa iliyopita, saa tano usiku, alipokuwa akitoka katika Msikiti wa Jabal Hald.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas, alisema jana kuwa, mtuhumiwa huyo ni mkazi wa Sekei na anaendelea kushikiliwa.
“Mtuhumiwa tunamshikilia hadi upelelezi utakapokamilika. Tunasubiri majibu kutoka kwa Mkemia Mkuu wa Serikali ili kubaini kama kweli kimiminika hicho kilikuwa tindikali,” alisema.
Kwa mujibu wa Sabas, sheikh huyo pia ni Imamu wa Msikiti wa Jabal Hald, ulioko eneo la Kwa Mrombo.
Alisema mkasa huo ulimpata wakati akitoka kusalisha sala ya Tarawehe, ambapo alipofika nyumbani kwake alitoka nje kwenda kujisaidia, ndipo ghafla aliposikia kishindo cha mtu aliyekuwa amebeba kikombe chenye maji na kumwagia usoni.
Mganga Mkuu wa mkoa, Frida Mokiti, alithibitisha kulazwa kwa sheikh huyo katika Hospitali ya mkoa ya Mount Meru na hali yake inaendelea vizuri.
Wakati huo huo, mkazi wa  Olmatejo, Zainabu Maulid (25), anashikiliwa akituhumiwa kughushi shahada ya kupigia kura yenye namba 32468790, aliyojaribu kuitumia juzi, kupiga kura katika kata ya Elerai.
Katika tukio lingine, bweni la Shule ya Sekondari ya Diozon, inayomilikiwa na Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Arusha liliteketea moto.
Sabas alisema tukio hilo lilitokea juzi, saa 1.30 usiku. Alisema bweni hilo lilikuwa na wanafunzi 142, ambao mali za zimeteketea.
Chanzo cha moto huo alisema ni hitilafu ya umeme.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru