Tuesday 16 July 2013

Bulembo awashika pabaya watendaji shule za Jumuia


NA RODRICK MAKUNDI, MOSHI
MWENYEKITI wa Jumuia ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdallah Bulembo, ameagiza watendaji wote waliosababisha madeni katika shule zinazomilikiwa na Jumuia hiyo, wakamatwe.

Bulembo, alitoa agizo hilo juzi, katika ziara yake mkoani ya kukagua uhai wa Chama na Jumuia zake sambamba na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM.
Alisema wote waliohusika kufanya hujuma hiyo, wasionewe haya, bali waamatwe na kuchukulia hatua kali za kisheria.
Bulembo, alisema hayo baada ya kusomewa taarifa ya Jumuia hiyo mkoani Kilimanjaro, ambapo pamoja na mambo mengine, ilielezwa kuwa shule nane kati ya 11 zinakabiliwa na madeni yanayofikia sh.milioni 800.
Kufuatia taarifa hiyo, Bulembo alisema hatakuwa tayari kupokea madeni hayo mpaka wahusika watakapokamatwa ili watoe maelezo kwa uzembe walioibebesha Jumuia hiyo mzigo huo.
Taarifa hiyo ilisema deni hilo linatokana na makato ya watumishi katika shule hizo ikiwemo ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), kutowasilishwa kwenye mamlaka hizo.
“Haiwezekani madeni haya yajionyeshe kwenye taarifa wakati tayari yalikatwa na ilipaswa yawe yamewasilishwa kwenye mamlaka zinazohusika, na mnaposema wahusika wameacha kazi, lazima waje wajieleze, naagiza wakamatwe na wafikishwe mahakamani,” alisema.
Alisema atahakikisha wote waliosababisha madeni hayo wanakamatwa.
Naye Menyekiti wa Jumuia Mkoa wa Kilimanjaro  Festo Kilawe, alisema deni hilo  linahusisha malimbikizo ya mishahara, makato ya NSSF na TRA.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru