Friday 19 July 2013

Madudu ya watumishi hadharani


NA MWANDISHI WETU
TUME ya Utumishi wa Umma imebaini madudu katika utendaji wa watumishi wa umma, ikiwemo kuzembea katika kuchukua hatua za kinidhamu kwa wanaoboronga kazi.
Kuchelewa kuchukua hatua kumesababisha baadhi ya watumishi kufanya makosa na kuendelea na kazi.
Tume imebaini tukio la mtumishi kutoroka kwa siku 200 huku akiendelea kulipwa mshahara.
Madudu hayo yamebainika baada ya viongozi wa tume kufanya ziara katika mikoa ya Dar es Salaam na Pwani, ambako walizungumza na waajiri na watumishi wa umma wa kada mbalimbali.
Mwenyekiti wa tume, Jovin Kitambi, alisema hayo jana alipozungumza na waandishi wa habari mjini Dar es Salaam, kuhusu ziara hiyo, iliyohusisha pia wakala 37 za serikali.
Alisema tume ilifanya ukaguzi kwa taasisi 42 kuangalia uzingatiaji sheria, kanuni na utaratibu katika maeneo ya ajira, upandishwaji vyeo, nidhamu, likizo za watumishi na upimaji wa wazi wa utendaji wa kazi kwa watumishi (OPRAS).
Kitambi alisema wamebaini  changamoto nyingi, ikiwemo baadhi ya waajiri na mamlaka za ajira na nidhamu kutozingatia sheria katika kushughulikia usimamizi wa rasilimali watu.
Changamoto nyingine ni watumishi kuchelewa kupandishwa vyeo na kuthibitishwa kazini na mashauri ya nidhamu kuendeshwa bila kufuata utaratibu.
“Kwa mfano mamlaka ya nidhamu kutochukua hatua pale mtumishi anapothibitika kufanya makosa, mtu anatoroka kwa siku 200 na anaendelea kulipwa mshahara,” alisema.
Akifafanua kuhusu watumishi kusimamishwa na kupumzishwa kazi, Naibu Katibu wa Tume, Idara ya Utumishi wa Serikali za Mitaa, Richard Odongo, alisema kanuni ya 38, kanuni ndogo ya nne ya utumishi wa umma imeweka wazi suala hilo.
Odongo alisema mtumishi akisimamishwa kazi anapaswa kulipwa nusu mshahara, lakini akipumzishwa anapaswa kulipwa mshahara na haki zake zote.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru