Monday 15 July 2013

Mbeki: Mandela atarejea nyumbani


JOHANNESBURG, Afrika Kusini
RAIS wa zamani wa Afrika Kusini, Thabo Mbeki, amesema anaamini Rais wa kwanza Mzalendo wa nchi hiyo, Nelson Mandela, ataruhusiwa kutoka hospitalini.

Mbeki, aliyekuwa Makamu wa Rais katika serikali ya Mandela, alisema hayo mwishoni mwa wiki alipoalikwa kwenye hafla maalumu iliyoandaliwa na chama tawala cha Afrika Kusini cha ANC.
Kwa mujibu wa Mbeki, amemtembelea Mandela mara kadhaa hospitalini alikolazwa na kwamba, hali yake imeimarika kiasi cha kuweza kuruhusiwa kutoka katika hospitali ya Pretoria alikolazwa tangu Juni 8, mwaka huu.
Kwa upande wake, Graca Machel, ambaye ni mke wa Mandela, hivi karibu alikaririwa akisema hana hofu na hali ya kiongozi huyo kama ilivyokuwa wiki kadhaa zilizopita.
Graca alisema Mandela anaendelea vizuri kutokana na juhudi zinazofanywa na madaktari wanaomhudumia na kwamba, anaamini anaweza kuruhusiwa kutoka hospitali.
Baadhi ya marafiki na watu walio karibu na Mandela waliomtembelea hospitalini walisema bado anapumua kwa msaada wa mashine.
Wiki iliyopita Denis Goldberg, rafiki wa karibu wa Mandela  alipinga taarifa zilizotolewa kwenye vyombo vya habari kuwa hali ya kiongozi huyo ilikuwa mbaya na kwamba, familia yake ilikuwa ikiangalia  uwezekano wa kuondoa mashine inayomsaidia kupumua.
“Mpiganaji Mandela anaendelea vizuri. Taarifa zinazotolewa kuhusu afya yake kuwa mbaya sana si za kweli,” alisema.
Goldberg aliyewahi kufungwa miaka 22 jela katika harakati za ukombozi wa nchi hiyo, alisema alipomtembea Mandela hospitalini licha ya kumkuta mgonjwa, alikuwa akijitambua na kujaribu kuzungumza.
Mbeki ndiye mrithi wa Mandela baada ya kustaafu mwaka 1999, na kuwa rais wa pili mweusi wa nchi hiyo.
Mandela alilazwa hospitalini hapo baada ya kuugua magonjwa mbalimbali, ikiwemo wa mapafu. Afya yake imekuwa ikibadilika mara kwa mara.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru