Friday 19 July 2013

Tanzania kufikia malengo ya chanjo


Na Mwandishi Wetu
SHIRIKA la Afya Duniani (WHO), limesema Tanzania ni nchi inayotarajiwa kufikia malengo matano ya chanjo ifikapo 2020.
WHO imesema vigezo ambavyo Tanzania inaweza kujivunia ni kutokomeza polio, kufikia malengo ya chanjo na kupunguza vifo vya watoto wachanga.
Mwakilishi wa WHO nchini, Dk. Rufaro Chatora, alisema hayo jana, katika hafla ya kukabidhi magari 24 kwa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii.
Alisema shirika hilo litaendelea kushirikiana na serikali katika kuhakikisha malengo ya mpango kazi wa chanjo yanafanikiwa.
Dk. Chatora alisema magari hayo yana thamani ya sh. bilioni moja na kwamba, 22 yatapelekwa wilayani kwa ajili ya kusambaza chanjo.
Magari mawili alisema yatapelekwa Bohari Kuu ya Dawa (MSD).
Kwa upande wake, Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Hussein Mwinyi, alisema taifa linaendelea kufanya vizuri katika huduma za chanjo.
Alisema asilimia 90 ya watoto wamepatiwa chanjo na kwamba, serikali itaendelea kuboresha huduma za afya.
Dk. Mwinyi aliishukuru WHO kwa msaada huo na kuahidi kuyatumia magari hayo kwa malengo yaliyokusudiwa.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru