Sunday 7 July 2013

JK: Michezo itumike kujenga umoja wetu


ATHANAS KAZIGE NA MOHAMMED ISSA
RAIS Jakaya Kikwete, amewataka Watanzania kuimarisha umoja, amani na upendo miongoni mwao kupitia michezo ili kujenga taifa lenye mshikamano.
Pia, alisema kukataa kugawanyika kwa misingi ya dini au siasa kutoka kwa baadhi ya watu wenye nia mbaya wanaotaka kuvuruga amani nchini.
Rais Kikwete alitoa rai hiyo alipokuwa mgeni rasmi katika tamasha la Matumaini lililofanyika jana Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Alisema michezo ina fursa nzuri ya kuimarisha umoja wa nchi na amefurahishwa na lengo la tamasha la matumaini kwa kuweka umoja bila ya ubaguzi, dini, rangi au kabila.
Rais Kikwete alisema kuwa watu wanaopita mitaani kubaguwa watu kwa misingi ya dini au siasa, wamefilisika na hawana hoja mbele ya jamii.
"Siasa siyo chuki na ndiyo maana Ngeleja na Zito wako upande mmoja wa timu ya Simba na Halima Mdee na Misanga wanacheza Yanga," alisema Rais Kikwete.
Alisema amefurahishwa na hatua ya waandaji kutumia sehemu ya mapato kujenga mabweni ya shule nane nchini.
Mabweni hayo yatajengwa katika shule za mikoa ya Mwanza, Mara, Tanga, Lindi, Kigoma na Dodoma. Pia, alitoa pongezi kwa wabunge waliofika uwanjani katika tamasha hilo.
Wakati huo huo, Rais Kikwete, alipuliza filimbi ya kuanza mchezo wa soka kati ya wabunge wanaoshabiki klabu za Yanga na Simba.
Katika mchezo huo ambao mwamuzi alikuwa, Athumani Kazi, maelfu ya mashabiki waliojitokeza uwanjani waliangua vicheko baada ya kushuhudia miamba hiyo 'ikimenyana' vikali.
Simba ilikosa nafasi kadhaa za kufunga kupitia kwa Kassim Majaliwa na Mwigulu Nchemba alishindwa kuing'arisha Yanga licha ya kuingia na mpira ndani ya eneo la hatari.
Simba: Idd Azan, Onesmo Laulau, Abeid Kikula, Adam Malima, William Ngeleja, John Kirumbi, Kassim Majaliwa,
Amos Makala, Hamis Kigwangala, Aziz Abdul na Halifa Halifa.
Yanga: Said Zuberi, Abdallah Haji, Godfrey Zambi, Poo Chimba, Cris Kamanyere, Said Mtanda, Danstan Kitandula, Ahmed Ngwali, Mwigulu Nchemba, Faki Mjaka na Mahmoud Mgimwa.

&&&&&&&&&&

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru