Tuesday 2 July 2013

Mbowe amuumbua Dk. Slaa


Na Mwandishi Wetu
HALI ya sintofahamu juu ya misimamo inayotolewa na uongozi wa juu wa CHADEMA inaendelea kukinzana mara kwa mara, ambapo sasa Mwenyekiti wa Chama hicho, Freeman Mbowe, anaonekana kumgeuka Katibu Mkuu wake, Dk. Wilbroad Slaa.
Hatua hiyo ilitokana na uamuzi wa Mbowe kushiriki dhifa ya kitaifa iliyoandaliwa na rais Jakaya Kikwete kwa ajili ya Rais wa Marekani, Barack Obama, juzi, usiku, IKulu, ambapo awali Dk. Slaa alisema hawatahudhuria.
Dk. Slaa alitoa msimamo huo siku moja kabla ya Rais Obama kuwasili nchini kwa ziara ya kikazi ya siku mbili ilimalizika jana na Rais Obama kurejea nchini mwake.
Akizungumza na gazeti linalomilikiwa na familia ya Mwenyekiti wake (Tanzania Daima), Dk. Slaa alisema CHADEMA, haitashiriki kwenye ziara ya Rais wa Marekani, kwa kuwa hawajaalikwa.
Dk. Slaa alisema hawawezi kuhudhuria ziara ambayo hawakualikwa, na kwamba serikali ndiyo yenye jukumu la kuwaalika watu mbalimbali kwa kuwa yenyewe ndiyo mwenyeji wa Rais Obama.
Alisema hadi kufikia jana jioni, hawakuwa na barua au taarifa ya kiofisi inazoonyesha kualikwa kwao katika ziara hiyo.
Sisi hadi leo (juzi) hatujapewa taarifa yoyote ya kiofisi, kwa hiyo hatuwezi kushiriki, kwani hatujui lolote, tupo kama Watanzania wengine tu,î alisema Dk. Slaa kuliambia gazeti hilo.
Katibu mkuu huyo alisema anashangazwa na usiri wa serikali kuhusu mwaliko wa CHADEMA ambacho ni chama kikuu cha upinzani nchini.
Sisi ni chama kikuu cha upinzani nchinii, hatujaambiwa Obama anakuja kufanya nini na sisi hatujui, lakini pia hatujaalikwa, hatuwezi kwenda sehemu ambayo hatukualikwa,î alisisitiza Slaa.
Hata hivyo, kauli hiyo ilionekana kwenda kinyume kutokana na Mbowe kushiriki dhifa hiyo ya kitaifa iliyoandaliwa na serikali kwa Rais Obama, huku akiwa ameandamana na baadhi ya wabunge wa chama hicho.
Wabunge hao ni pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA (Bara), Zitto Kabwe na Ezekiel Wenje ambaye ni mbunge wa Nyamagana ambaye pia ni waziri kivuli wa mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa.
Kushiriki kikamilifu kwenye dhifa hiyo kwa viongozi hao waandamizi wa CHADEMA wakiongozwa na Mbowe, kumeelezwa na baadhi ya wanachama wa chama hicho kuwa Dk. Slaa amekuwa akifanya mambo kwa kukurupuka.
Mmoja wa wanachama aliyezungumza na UHURU akiwa makao makuu ya chama hicho, Dar es Salaam kuhusiana na suala hilo alisema mara nyingi Slaa amekuwa akitolea matamko masuala mbalimbali ya chama hicho kutokana na utashi wake, lakini si msimamo wa chama.
“Mambo kama haya ndio yanayoibua migogoro isiyo ya lazima ndani ya chama kwa kuwa chama kinakuwa na wasemaje wengi kuliko kawaida... leo utamkuta Kigaila (Benson) anasema hivi, mara John Mnyika vile,” alisema mwanachama huyo ambaye hakutaka jina litajwe.
Alisema hali hiyo imekuwa ikimfanya Dk. Slaa mara kadhaa kutoa kauli ambazo muda mwingine amekuwa akizigeuka, ambapo awali aliwahi kusema hawamtambua Rais Kikwete kwa kuwa ameingia madarakani kwa wizi wa kura baada ya kumalizika kwa uchaguzi mkuu wa 2010.
Alisema kauli hiyo ilionekana kukinzana na yeye mwenyewe, ambapo baada ya muda alikwenda Ikulu kuonana na Rais Kikwete wakati akipeleka maoni ya CHADEMA juu ya rasimu ya mabadiliko ya katiba baada ya kuvitaka vyama vya siasa kuonana naye Ikulu kuzungumzia mambo hayo.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru