Tuesday 16 July 2013

Ni msimu wa neema


JUMANNE GUDE NA
RACHEL KYALA
SERIKALI imesema hali ya chakula kwa mwaka huu ni nzuri, kutokana na mavuno ya kuridhisha katika mikoa 19 nchini.
Msemaji wa Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika, Richard Kasuba, alisema hayo jana, alipozungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Dar es Salaam.
Kasuba alisema upatikanaji wa vyakula sokoni unaridhisha na bei zinaendelea kushuka kadri msimu wa mavuno unavyoendelea.
Hata hivyo, serikali imewaasa wakulima kutouza chakula chote na kuhakikisha wanaweka akiba ya kutosha kwa ajili ya matumizi ya familia.
Alisema Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA), umeanza kununua nafaka kwa ajili ya kuongeza hifadhi ya chakula, ambapo unatarajia kununua tani 200,000 kutoka kwenye maeneo yenye ziada, hususan vijijini.
Serikali imewataka wakulima kuuza nafaka zinazokidhi vigezo vya ubora, kama vile kukaushwa vizuri, kutokuwa na takataka, zisiwe na punje zilizovunjika au kuliwa na wadudu, zenye rangi tofauti na ambazo hazijaathiriwa na ugonjwa wa mahindi.
Kasuba alisema NFRA itanunua chakula kwa kuzingatia gharama za uzalishaji na bei ya soko katika eneo la ununuzi, ili kurudisha gharama za uzalishaji kwa mkulima.
Alisema majukumu makuu ya wizara ni kuhakikisha nchi inakuwa na chakula cha kutosha, na kilimo kinachangia kikamilifu katika ukuaji wa uchumi wa taifa na kuondokana na umasikini.
Naye Mkurugenzi wa Usalama wa Chakula, Karim Mtambo, alisema ili kutunza mazao yasiharibiwe, wizara imeweka ramani ya aina ya udongo wa kila eneo na aina ya mbolea inayofaa kutumika.
Pia kushauri wakulima kujikita katika kilimo mseto ili kutunza rutuba.
Mtambo alisema ili kukabiliana na ugonjwa unaoathiri mahindi, wizara imeamua kutokuingiza mbegu za nafaka kutoka nchi jirani.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru