Tuesday 16 July 2013

Dawa za mabilioni kuteketezwa moto


Na Theodos Mgomba, Dodoma
WILAYA ya Kondoa inatarajia kuteketeza dawa za aina mbalimbali zilizoisha muda wake zenye thamani ya sh. bilioni 80.
Hayo yalisemwa jana na Mfamasia Mkuu wa Wilaya hiyo, Said Mayanja, katika mkutano wa uhamasishaji wa wananchi kujiunga na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF).
Alisema tayari halmashauri imeshaoomba kibali cha kuteketeza dawa hizo toka Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii.
Mfamasia huyo, alisema kati ya dawa zilizoisha muda wake ni pamoja za kupunguza makali ya virusi vya ukimwi (ARVs) na malaria.
Kwa mujibu wa Mayanja, wilaya hiyo ina dawa nyingi zilizoimeisha muda wake, lakini wanasubiri utaratibu wa kuteketeza.
Alisema baadhi ni za mwaka 2000, lakini kutokana na utaratibu wa kuteketeza kuwa mrefu, dawa hizo bado zinahifadhiwa.
“Tumeshaandika barua Wizara ya Fedha kuomba fedha kwa ajili ya kazi hiyo na tayari mkurugenzi wa halmashauri ameshasaini,”alisema.
Mayanja alisema moja ya sababu ya kuwepo kwa shehena kubwa ya dawa hizo, ni kutokana na Bohari ya Dawa (MSD), kuleta dawa ambazo hazilingani na mahitaji husika.
Alisema ili kuondokana na tatizo hilo,  tayari wameanzisha mfumo wa kuunganisha wahudumu wa vituo vyote vya afya na ofisi yake, ambapo sasa wanapata taarifa za uwepo wa dawa za kila mwezi.
Mfamasia huyo, alisema mfumo huo utasaidia kwa kiasi kikubwa katika kuwasilisha maombi ya dawa kwa wakati kwenye ofisi za MSD.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru