Monday 29 July 2013

Serikali yadhibiti ‘mchwa’ Utumishi


NA KHADIJA MUSSA
MFUMO mpya wa taarifa na ulipaji mishahara kwa watumishi wa umma, umewezesha kukatwa mirija ya ulaji kwa baadhi ya watendaji waliokuwa wakitafuna mabilioni ya shilingi kila mwezi.
Kuanzishwa kwa mfumo huo kumeifanya serikali kudhibiti tatizo la mishahara hewa kwa watumishi.
Awali, watumishi waliofariki dunia waliendelea kulipwa mishahara na kuchukua mikopo, jambo lililokuwa likifanywa na watendaji wasio waadilifu.
Mfumo huo pia umezima safari za maofisa waliokuwa wakisafi kutoka mikoani kwenda Dar es Salaam kuwasilisha taarifa za watumishi, ambao walikuwa wakilipwa posho, hivyo kuiongezea mzigo serikali.
Tangu kuanza kutumika kwa mfumo shirikishi wa taarifa za kiutumishi na mishahara katika utumishi wa umma (HCMIS),
serikali inaokoa sh. bilioni 1.5 kila mwezi.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano katika Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Florence Temba, alisema mfumo huo pia umepunguza tatizo la malimbikizo ya mishahara kwa watumishi.
Temba alisema umesaidia kurahisisha kuingizwa kwa taarifa za watumishi wapya kwa ajili ya utaratibu wa malipo katika kipindi cha muda mfupi, tofauti na ilivyokuwa awali.
Alisema mfumo huo umesaidia kuimarisha usimamizi wa rasilimali watu na mishahara katika utumishi wa umma.
“Kabla ya mfumo huu kuwepo, taarifa nyingi za watumishi zilipotea na kuleta usumbufu kwa wengi kufuatilia, ilichukua miezi sita hadi 12 kuchelewesha kuingiza watumishi wapya katika orodha ya malipo. Kwa kutumia HCMIS kazi hufanyika kwa dakika 30,” alisema.
Temba alisema mfumo huo pia umepunguza tatizo la malimbikizo ya mishahara ya watumishi wa umma linalosababishwa na kuchelewesha mishahara ya watumishi wapya au wanaopandishwa vyeo.
Alisema ukokotoaji wa malimbikizo ya mishahara ulianza Mei hadi Novemba, mwaka jana,  ambapo malimbikizo ya sh. bilioni 7.9 ya watumishi 15,677 yalifanyiwa kazi.
Kupitia mfumo huo, alisema umerahisisha malipo ya mishahara na stahili kwa watumishi wa umma na kwa wakati, na umewezesha kuondoa watumishi takriban 34,645 kwenye orodha ya malipo ya mishahara kutokana na sababu mbalimbali tangu mwaka 2010 hadi Juni 30, mwaka huu.
Temba alisema wizara, idara zinazojitegemea, wakala za serikali, sekretarieti za mikoa, mamlaka za serikali za mitaa na taasisi za serikali zinazopata ruzuku kwa asilimia 100 kutoka HAZINA zinapaswa kutumia mfumo huo katika kusimamia rasilimali watu na mishahara.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru