Wednesday 17 July 2013

Maghorofa yaburuza vigogo kortini Dar


NA FURAHA OMARY
TAASISI ya Kuzuia na Kupambana
na Rushwa (TAKUKURU), imewaburuza kizimbani vigogo wanne wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) na Wizara ya Fedha, wakituhumiwa kwa matumizi mabaya ya madaraka na ubadhirifu.
Vigogo hao walifikishwa jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, na kusomewa mashitaka mbele ya mahakimu tofauti.

Waliofikishwa mahakamani kutoka TBA ni aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji, Makumba Kimweri na Msanifu Mkuu wa wakala huo, Richard Maliyaga.
Kutoka iliyokuwa Wizara ya Fedha na Uchumi, waliopandishwa kizimbani ni Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Ununuzi, Ernest Mwakitalu na Ofisa Ugavi, Liipu Nelingwa.
Kimweri na Maliyaga walipandishwa kizimbani mbele ya Hakimu Mkazi Sundi Fimbo, wakikabiliwa na mashitaka matano ya matumizi mabaya ya madaraka.
Wanadaiwa kukiuka madaraka katika utoaji kibali cha ujenzi wa jengo la ghorofa 15 kwenye viwanja namba 45 na 46, vilivyoko mtaa wa Chimara, wilayani Ilala.
Akiwasomea mashitaka, mwendesha mashitaka kutoka TAKUKURU, Leonard Swai, alidai Kimweri, Agosti 6, 2007, katika ofisi za wakala huo wilayani Ilala, akiwa Mkurugenzi Mtendaji kwa nia ovu alitumia madaraka yake vibaya kwa kutia saini hati ya makubaliano namba TBA/JVA/DSM/ROI/001 kati ya TBA na Royalle Orchard Inn Ltd.
Swai alidai hati hiyo ilianzisha uhusiano kati ya serikali na sekta binafsi kwa ajili ya ujenzi na umiliki wa jengo hilo bila kufanya upembuzi yakinifu kuhusu mradi huo, hivyo kuipatia manufaa Royalle.
Kimweri anadaiwa siku hiyo, katika ofisi za TBA, alitumia madaraka vibaya kwa kutia saini hati ya makubaliano yenye namba TBA/JVA/DSM/ROI/002, kati ya wakala huo na Royalle ili kuanzisha uhusiano kati ya serikali na sekta binafsi kwa ujenzi na umiliki wa ghorofa katika kiwanja namba 46.
Maliyaga anadaiwa Julai 21, 2008, katika ofisi za TBA, akiwa Msanifu Mkuu, kwa nia ovu alitumia vibaya madaraka yake na kutoa kibali cha ujenzi namba TBA/BP/155 kuruhusu Royalle kujenga jengo la biashara la ghorofa 15 katika viwanja namba 45 na 46, bila kupata kibali kutoka kwa Idara ya Mipango Miji ya Manispaa ya Ilala.
Pia anadaiwa Aprili 9, 2009, alitumia madaraka vibaya kwa kutoa kibali cha ujenzi namba TBA/BP/155(a) kwa Royalle kuongeza jengo la biashara kutoka ghorofa 15 hadi 18, bila kupata kibali kutoka mamlaka husika.
Kimweri na Maliyaga wanadaiwa katika tarehe tofauti kati ya Agosti 6, 2007 na Aprili 9, 2009, kwenye ofisi za TBA, wakitekeleza majukumu yao, walitumia madaraka vibaya kwa kutoa kibali kwa Royalle kujenga jengo la biashara bila kibali na kubadilisha matumizi ya ardhi.
Washitakiwa walikana mashitaka, ambapo Swai alidai upelelezi umekamilika na hana pingamizi kuhusu dhamana.
Hakimu Sundi alitoa masharti ya dhamana akiwataka kila mmoja awe na wadhamini watatu, ambao ni wafanyakazi wa serikali, watakaoitia saini dhamana ya sh. milioni 50. Kesi itatajwa Agosti mosi, mwaka huu, kwa usikilizwaji wa awali.
Katika hatua nyingine, Mwakitalu na Liipu, walipandishwa kizimbani mbele ya Hakimu Mkazi Nyigulila Mwaseba, wakishitakiwa kwa makosa 10.
Wanadaiwa kula njama, kutumia nyaraka kwa nia ya kumdanganya mwajiri, matumizi mabaya ya madaraka, kughushi, ufujaji na ubadhirifu wa sh. milioni 19.8 na kuisababishia mamlaka husika hasara ya kiasi hicho cha fedha.
Swai akiwasomea mashitaka, alidai kesi hiyo inawakabili washitakiwa wanne lakini mahakamani wapo Mwakitalu na Liipu, kwa kuwa wengine hawajapatikana.
Alidai Mwakitalu, Liipu na wenzao ambao hawapo mahakamani, kati ya Juni na Julai, 2009, Dar es Salaam, walikula njama ya kutenda kosa la kutumia nyaraka kwa nia ya kumdanganya mwajiri.
Mwakitalu na mwenzake, ambaye hajafikishwa mahakamani, wanadaiwa Juni, 2009, katika Wizara ya Fedha na Uchumi, walitia saini na kutumia nyaraka ya ununuzi ya Juni 29, 2009, ikiwa na maelezo ya uongo kuonyesha kampuni ya AND-LINE (2000) International Co imepewa idhini ya kutoa huduma ya habari.
Maelezo hayo yalionyesha  walitakiwa kutoa habari nne kwenye vituo vya televisheni, nane kwenye vituo vya redio, tano kwenye magazeti, picha 10 na kipindi cha dakika tano kuhusu wizara hiyo kurushwa kwenye vituo vinne vya televisheni.
Kazi hizo zingefanyika wakati wa Maonyesho ya 33 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (DITF), katika Viwanja vya Mwalimu J.K Nyerere, kuanzia Juni 28 hadi Julai 10, 2009.
Washitakiwa wanadaiwa kughushi, kufuja na kufanya ubadhirifu wa sh. milioni 19.8, walizopewa na wizara kwa ajili ya vyombo vya habari wakati wa maonyesho hayo. Pia wanadaiwa kuisababishia hasara mamlaka husika ya kiasi hicho cha fedha.
Washitakiwa walikana mashitaka, ambapo Swai alidai upelelezi umekamilika.
Hata hivyo, aliomba shauri hilo litajwe ili wapate muda wa kuwatafuta washitakiwa ambao hawapo mahakamani.
Hakimu Nyigulila alitoa masharti ya dhamana, akimtaka kila mshitakiwa kuwa na wadhamini wawili wa kuaminika, watakaotia saini bondi ya sh. milioni tano. Kesi itatajwa Agosti 15, mwaka huu.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru