Monday 29 July 2013

Mchungaji awashukia wavaa vimini kanisani


Na Frank Kibiki, Iringa
MCHUNGAJI wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheli Tanzania (KKKT), Usharika wa Iringa mjini, Huruma Bimbiga, amepiga marufuku mavazi ya aibu ambayo yanaonyesha sehemu za miili yakiwemo mabega kwa maharusi, wasimamizi na wapambe wao kanisani hapo.
Akizungumza na Uhuru, Mchungaji Bimbiga alisema kufuatia baadhi ya maharusi kuvaa mavazi yasiyo ya kimaadili, wameamua kuanzisha somo la kuwaelimisha maharusi juu ya mavazi yafaayo kuvaliwa kanisani.
Mchungaji Bimbiga alisema elimu hiyo huitoa katika mafundisho ya ndoa.
Alisema lengo ni kuwataka watambue kuwa siku ya harusi wakivaa vibaya, wakikataliwa kuingia kanisani, wasione kama wananyanyaswa na watumishi wa Kanisa.
Alisema kufuatia hali hiyo, wamejiwekea utaratibu wa kuwavalisha kanga au kuwakatalia kuingia kanisani wale wanaovaa hovyo.
“Ni aibu na ni kinyume na maadili ya kanisa kwa mabinti zetu kuvaa nguo zinazoonyesha miili yao.
“Japo wao wanadhani ni fasheni, lakini kwetu hatupo tayari kuongoza Ibada ya ndoa wakati mavazi yanayovaliwa hayatubariki,” alisema Bimbiga.
Alisema, wakati wa ibada za kawaida wasichana wengi huvaa mavazi ya heshima, tatizo kubwa huwa wakati wa ibada za ndoa. Wengi wao huvaa magauni yanayoonyesha miili yao.
Alitoa wito kwa wazazi kuwaelimisha mabinti namna ya kuvaa mavazi ya heshima.
Alisema hiyo pia ni moja ya kazi ya kuwajengea maadili ndani ya jamii.
Mmoja wa wazee wa kanisa hilo, Peter Sanga, alisema miongozi mwa kazi zinazopaswa kufanywa na viongozi wa Kanisa, ni kuangalia nidhamu ya mavazi kwa waumini wake.
“Binafsi, mtu akija na nguo ya ajabu, awe mwanamke au mwanaume, siwezi kumruhusu aingie kanisani, ni bora nimvishe kanga au nimwambie ukweli akabadilishe ili Neno la Mungu litimie,” alisema Sanga.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru