Tuesday 26 August 2014

Kamanda Sabas amuumbua Lema



NA SHAABAN MDOE, ARUSHA
KAMANDA wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas amemzima mbunge wa Arusha, Godbless Lema kwa kumweleza kuwa jeshi hilo haliwajibiki kutoa taarifa za uhalifu kwa Waziri Kivuli wa Wizara ya Mambo ya Ndani.
Kauli ya Kamanda Sabas imetokana na Lema kudai kuwa jeshi hilo haliwasilishi kwake taarifa za matukio ya kihalifu yanayotokea Arusha na kwamba, hiyo inaonyesha ni dharau.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kamanda Sabas alisema polisi hawawajibiki kutoa taarifa za kihalifu kwa Lema na kwamba, taarifa za kihalifu zinatolewa kwa Waziri kamili wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, ambayo inaongozwa na Mathias Chikawe.

“Hatushughuliki na Waziri Kivuli wakati mwenye dhamana kisheria yupo, hayo mambo ya vivuli ni huko huko bungeni na sio kwetu. Hatuna utaratibu wa kutoa taarifa zetu kwa waziri kivuli wala mbunge,” alisema Kamanda Sabas.

Hivi karibuni, akihutubia mkutano wa hadhara katika Viwanja vya Samunge, Lema alidai hashirikishwi kwenye uamuzi wa kuanzisha mfuko kuisaidia polisi kupambana na uhalifu jijini hapa.
Kwa mujibu wa Sabas, alisema si mara ya kwanza kwa Lema kulitupia lawama jeshi hilo kwa lengo la kulichafua mbele ya jamii ili apate umaarufu.
Alisema baada ya matukio ya kulipuliwa kwa mabomu katika maeneo mbalimbali ya jiji la Arusha, likiwemo la mkutano wa CHADEMA uliofanyika uwanja wa Soweto, Lema alilituhumu jeshi hilo kuhusika na mlipuko huo.
Pia alisema Lema alishawahi kuharibu uhusiano uliokuwepo baina yake na jeshi hilo na kwamba, siku zote hakubali kazi inayofanywa na jeshi hilo.
Alisema Lema anatakiwa kujiuliza kwanini kama mwakilishi wa wananchi hajashirikishwa katika kuanzisha mfuko maalumu wa fedha kwa ajili ya ulinzi wa raia na mali zao na sio kulilaumu jeshi la polisi kuwa halijamshirikisha katika mpango huo.
Kamanda Sabas alisema uamuzi wa kuanzishwa kwa mfuko huo hauakutolewa na jeshi la polisi na kwamba, ni wananchi wenyewe waliohudhuria katika mkutano wa polisi na wadau wa usalama.
Alisema mkutano huo ulifanyika katika ukumbi wa bwalo la polisi, Agosti 14, mwaka huu.

RPC Liberatus Sabas - Arusha
“Ni vyema Lema akafahamu kuwa sisi sio tuliomba kuchangiwa hizo fedha bali wananchi ndiyo waliamua kuwepo kwa mfuko huo, hivyo ni vyema akawaulize anaodai kuwaongoza," alisema.

Hata hivyo, alimtaka Lema kuunga mkono juhudi hizo badala ya kuzipinga kwa maslahi yake binafsi.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru