Thursday 28 November 2013

‘Kampuni za simu ziache ukiritimba’


NA RABIA BAKARI
KAMPUNI za simu nchini, zimetakiwa kuungana katika matumizi ya minara ya mawasiliano na kuacha ukiritimba wa kila kampuni kutumia minara yake.

Agizo hilo lilitolewa jana mjini Dar es Salaam na Makamu wa Rais, Dk. Mohamed Ghalib Bilal, alipokuwa akizindua sherehe za maadhimisho ya miaka kumi tangu kuanzishwa kwa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA).
Alisema kushirikiana katika matumizi ya minara kutapunguza fedha za kigeni zinazotumika kuagiza minara hiyo, badala yake zitasaidia kusambaza huduma za mawasiliano sehemu mbalimbali ambazo bado hazijafikiwa.
Pia, alizitaka kampuni hizo zitoe fursa ya mafunzo na elimu ya kisasa ya mifumo mipya ya mawasiliano kwa wafanyakazi wake, ili waendane na kasi ya mabadiliko ya kiteknolojia.
Dk. Bilal aliipongeza TCRA kwa juhudi kubwa ya kuhakikisha sekta ya Teknolojia, Habari na Mawasiliano inapiga hatua kwa kasi kubwa na kuisisitiza kutunga sheria na kuweka mikakati ya usalama wa TEHAMA ikamilishwe mapema na wananchi wapewe elimu.
Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Dk. Makame Mbarawa, alisema juhudi za CCM, kupitia ilani zake za mwaka 2005 na 2010, zimesaidia ukuaji wa kasi wa sekta ya mawasiliano na kuchangia pato la taifa.
“Tanzania imeweza kupokea mawaziri, viongozi na wataalam kutoka nchi marafiki kama Kenya, Uganda, Burundi, Malawi, Botswana, Namibia, Msumbiji na Lesotho kwa ajili ya kujifunza na kubadilishana uzoefu katika kusimamia sekta ya mawasiliano nchini mwao,” alisema.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru