Tuesday 5 November 2013

Meneja adaiwa kumuunganishia umeme mchungaji wake


Na Jumbe Ismailly, Ikungi
WATU wawili, akiwemo Meneja wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) wilayani hapa, wanashikiliwa na polisi kwa tuhuma za wizi wa umeme kwa zaidi ya miezi miwili sasa.
Akizungumzia tukio hilo, Ofisa Usalama wa TANESCO Mkoa wa Singida, Damasi Gamba, alisema watu hao ni meneja huyo, Godfyer John na Mchungaji wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Kati, Usharika wa Ikungi, Mchungaji Paulo Misai.
Aidha, ofisa usalama huyo alisema mchakato wa kuwasaka watu wanaojiunganishia nishati hiyo ni endelevu, huku akiongeza watu wanaoishi kwenye maeneo ya pembezoni ndiyo wanaodaiwa kujihusisha zaidi na vitendo vya wizi huo.
Alisema hali hiyo imekuwa ikirudisha nyuma juhudi za shirika la kutoa huduma bora kwa wananchi, licha ya kuendesha oparesheni ya kuwakatia umeme wateja wanaodaiwa kutolipa ankara zao.
“Hivi karibuni tulimkamata mtu mmoja wilayani hapa kwa kujiunganishia umeme bila kufuata taratibu kupitia mita ya mtu, lakini akachimbia waya chini kwa chini hadi nyumbani kwake.
“Tulimkamata na kumfikisha kituo cha polisi kwa hatua zaidi za kisheria, ambapo hadi sasa anashikiliwa na polisi,” alisema ofisa huyo.
Akifafanua, kuhusu meneja huyo wa wilaya, Gamba alisema alikiri kuhusika kufanikisha wizi huo kwa kile klinachodaiwa kwamba ni kiongozi wake wa dini na jirani yake.
“Suala kama hili linapojitokeza, lazima kuwe na mfanyakazi wa TANESCO anayehusika na hujuma hizo au vishoka, ambao wamekuwa wakifanya makubaliano na kuchezea umeme kama hivi ilivyoonekana siku ya tukio,” alisema.
Kwa mujibu wa Gamba, kinachoonekana ni kwamba meneja huyo alihusika kumpelekea umeme mchungaji huyo, ingawa alikiti na kuwa hivi sasa anasubiri hatua nyingine za kinidhamu.
Kwa upande wa Mchungaji Misai, licha ya kukiri kukamatwa akitumia umeme kinyume cha taratibu, alisema alikuwa akisubiri kuunganishiwa umeme wa kwa mujibu wa taratibu za TANESCO.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru