Thursday 28 November 2013

NSSF yawafanyia tathimini watoa huduma



Na Theodos Mgomba, Dodoma
SHIRIKA la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF),  limeanza utaratibu wa kufanya tathimini  kwa watoa huduma ya fao la matibabu kwa wanachama wake.
Mkurugenzi Mkuu wa NSSF Dk. Ramadhan Dau, aliyasema hayo jana alipokuwa akitoa taarifa za awali katika Mkutano wa Sita wa watoa huduma ya matibabu wa Shirika hilo.
Dau, alisema kazi hiyo ya kufanya tathimini ya watoa huduma inafanywa kwa ushirikiano na Taasisi ya Pharm Acces International.
Alisema nia ya utafiti huo ni kuona uwezo wa vituo hivyo na utoaji wake wa huduma kwa wanachama hao ili kupunguza malalamiko, ikiwemo ukosefu wa vifaa tiba katika baadhi ya vituo husika.
“Baadhi ya Hospitali ambazo tumewapa kazi ya kutoa huduma kwa wanachama wetu, wamekuwa wakitoa huduma chini ya viwango tulivyotegemea, hivyo kusababisha malalamiko kwa wanachama wanapotaka huduma,” alisema Dk. Dau.
Mkurugenzi huyo, alisema imekuwa ikiwapa wasiwasi wanachama na kuwafanya baadhi yao kutojiunga na fao hilo.
Alisema mpaka sasa, kuna watoa huduma 375 wa vituo na hospitali mbalimbali  na wanachama waliojiunga na fao hilo kwa sasa wanafikia 102,089, toka kuanzishwa kwa fao hilo miaka saba iliyopita.
Hata hivyo, aliwatoa wasiwasi wanachama wa NSSF, kuwa kujiunga na fao hilo hakusababishi kukatwa pensheni yao siku ya mwisho, kwani katika makato ya sasa fao hilo nalo lipo.
Akifungua mkutano huo, Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudentia Kabaka, aliitaka NSSF kutoa elimu kwa wanachama wake juu ya kujiunga na fao hilo bila kuwachanganya au kuwalipisha mara mbili.
Alisema kwa sasa changamoto kubwa ni kwa wataalamu wa afya wanaotoa huduma kwa wanachama hao kuzingatia miiko ya taaluma ya fani ya utabibu wakati wote wakiwa kazini.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru