Tuesday 19 November 2013

Ujenzi kituo cha afya UDOM wakamilika


Na Theodos Mgomba, Dodoma.
UJENZI wa kituo cha uchunguzi wa kiafya kilichogharamiwa na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya(NHIF) katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) umekalimika kwa asilimia 96.
Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Idris Kikula, alisema kituo hicho kinatarajiwa kufunguliwa hivi karibuni na Rais Jakaya Kikwete.
Kwa mujibu wa Kikula, kitakuwa na uwezo wa kuchunguza magonjwa yote makubwa ambayo kwa sasa baadhi hayana uwezo wa kuchunguzwa nchini.
Alisema pamoja na kufunguliwa kwa kituo hicho, mfuko huo pia unatarajia kujenga hospitali kwa ajili ya kufundishia wanafunzi.
Alisema ujenzi huo utaanza hivi karibuni na hospitali hiyo itakuwa msaada mkubwa kwa wanafunzi wa Chuo cha Sayansi ya Afya, kwa kuwawezesha kupata uelewa mkubwa katika masomo yao.
Kitatoa pia huduma kwa wananchi wa kawaida na wale wa nje ya nchi.
Wakati huo huo; Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Zhengzhough cha nchini China, kimeanzisha kituo cha kufundishia lugha ya Kichina katika chuo cha UDOM.
Makamu Mkuu wa Chuo cha UDOM, alisema kilianzishwa mapema Februari mwaka huu.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru