Friday 8 November 2013

Vyakula, mavazi vyapanda bei


NA NJUMAI NGOTA
MFUMUKO wa bei kwa bidhaa za vyakula na mavazi umepanda kwa mwezi uliopita ikilinganishwa na Septemba, mwaka huu.
Vyakula vimepanda kutoka asilimia 6.1 hadi asilimia 6.3 na mavazi ya watoto kwa asilimia 0.4, mafuta ya taa kwa asilimia 2.1 na vifaa vya nyumbani vya usafi kwa asilimia 0.4.
Mkurugenzi wa Takwimu za Jamii wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Ephrahim Kwesigabo, alisema jana kuwa mfumuko huo umeongezeka kutokana na kasi ya bei za bidhaa na huduma kwa mwezi uliopita.
Kwesigabo alisema kuongezeka kwa bei kwa mwezi huo kumechangiwa na kuongezeka kwa mfumuko wa bei wa bidhaa za vyakula na bidhaa zisizo za vyakula.
Alisema mfumuko wa bei ya vyakula vya nyumbani na migahawa umeongezeka hadi asilimia 7.3 mwezi uliopita ikilinganishwa na asilimia 6.9 Septemba, mwaka huu.
“Kwa upande wa bidhaa zisizo za vyakula, kasi ya ongezeko la bei imekuwa kidogo hadi asilimia 6.1 Oktoba, mwaka huu, kutoka asilimia 6.0 Septemba, mwaka huu,”alisema.
Mkurugenzi huyo alisema baadhi ya vyakula vilivyochangia kwa kiasi kikubwa kuongezeka kwa mfumuko huo kwa kipimo cha mwezi ni unga wa mahindi kwa asilimia 1.5 na unga wa muhogo kwa asilimia 3.5.
Bidhaa nyingine na asilimia zake kwenye mabano ni nyama (1.2), kuku (3.7), samaki wabichi (4.1), samaki wakavu (9.0), dagaa (2.5), maziwa ya ng’ombe (1.2), matunda (2.9), nazi (2.6), viazi vitamu (4.2) na asali (5.0).
Alisema wataalamu wa uchumi duniani wanasema uwezo wa fedha katika kununua bidhaa na huduma una uhusiano na mwelekeo wa kipimo kinachotumika kupima mabadiliko ya bei za bidhaa na huduma zinazotumiwa na jamii.
Kwesigabo alisema kama vipimo vya bei vikipungua, uwezo wa fedha katika kununua bidhaa na huduma unaongezeka na inaonyesha kwamba mwelekeo imara kwa kipindi chote cha mwaka kutoka Januari hadi Oktoba, mwaka huu.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru