Thursday 14 November 2013

JK awalisi Colombo kwa mkutano wa CHOGM

NA MWANDISHI MAALUMU
RAIS Jakaya  Kikwete amewasili mjini Colombo, Sri Lanka,
kuhudhuria Mkutano wa Wakuu wa Serikali za Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Madola (CHOGM).
Taarifa iliyotolewa jana na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Dar es Salaam, ilisema Rais Kikwete ambaye anaandamana na mkewe Mama Salma  aliwasili jana mjini humo akitokea Dubai, Falme za Kiarabu, ambako aliwasili usiku wa jana akitokea nyumbani.
Mkutano huo wa siku tatu unaanza leo kwenye Ukumbi wa Mahinda Rajapaska Theatre katika eneo la Nelum Pokuna mjini Colombo, mji mkuu wa Sri Lanka. Mkutano huo utafunguliwa rasmi na Prince Charles, mtoto wa Malkia wa Uingereza kwa niaba ya mama yake, Malkia Elizabeth ambaye ndiye kiongozi wa Jumuia ya Madola, ambaye hata hivyo, hataweza kuhudhuria mkutano wa mwaka huu. Mara baada sherehe za ufunguzi, Rais Kikwete ataungana na viongozi wenzake kwa ajili ya vikao rasmi vya mkutano huo vitakavyofanyika kwenye Kituo cha Maonyesho ya Kumbukumbu cha Sirimavo Bandaranaike. Miongoni mwa shughuli kubwa za leo ni vikao viwili rasmi vya kwanza vya viongozi wa jumuia hiyo na majadiliano kati ya viongozi hao na viongozi wa vijana kutoka nchi wanachama wa Jumuia ya Madola.
Aidha, viongozi hao, akiwemo Rais Kikwete watahudhuria hafla rasmi ya makaribisho itakayoandaliwa na Katibu Mkuu wa Jumuia ya Madola, Kamalesh Sharma katika Ukumbi wa Bandaranaike Memorial International Conference Hall (BMICH).
Jana, Rais Kikwete na Mama Salma, walitarajiwa kuhudhuria hafla ya chakula cha usiku kitakachoandaliwa na Prince Charles na mkewe, The Duchess of Corwall, kwenye hoteli ya Cinnamon Lakeside.
Jumuia ya Madola ni umoja wa nchi zilizokuwa chini ya ukoloni na himaya ya Uingereza na nchi nyingine ambazo zenyewe ziliomba na kukubaliwa kujiunga na Jumuia hiyo, zikiwemo Msumbiji na Rwanda.
Jumuia ya Madola ina jumla ya nchi wanachama 53, zikiwemo nchi 18 za Afrika ambalo ni bara lenye wanachama wengi zaidi katika jumuia hiyo, nchi nane za Asia, 13 za Marekani na Caribbean, tatu za Ulaya na 11 za Pacific.
Pia, jumuia hiyo ina mchanganyiko wa nchi kubwa na ndogo, nchi 32 kati ya hizo zilihesabiwa kama nchi ndogo kwa maana ya kuwa na idadi ya watu milioni 1.5 au chini ya hapo.
Sri Lanka ambayo mpaka mwaka 1972 ilijulikana kwa jina la Ceylon, inajulikama rasmi kama Jamhuri ya Kidemosia ya Kisoshalisti ya Sri Lanka. Ni nchi kisiwa kilichoko Kaskazini mwa Bahari ya India na Kusini mwa pwani ya nchi ya India. Ni nchi yenye mipaka ya maji na India na Maldives.





Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru