Thursday 22 May 2014

Halmashauri zaagizwa kuwatengea maeneo ‘wamachinga’


TUMAINI MSOWOYA, DODOMA
SERIKALI imezitaka halmashauri zote za miji na majiji nchini, kuhakikisha zinatekeleza agizo la kutenga na kuyatangaza maeneo yote muhimu kwa ajili ya wafanyabishara ndogo ndogo, maarufu kwa jina la wamachinga.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, William Lukuvi, alisema hayo juzi bungeni mjini hapa wakati akijibu hoja za wabunge kuhusu mkakati wa serikali katika kuwasaidia wafanyabishara hao.
Lukuvi alisema serikali inatambua umuhimu wa wamachinga katika kukuza uchumi wa nchi na kwamba ilishatoa agizo la kutaka halmashauri zaote za miji na majiji kuhakikisha zinatenga maeneo hayo.
Alisema serikali ilishasikia kilio chao na kwamba, Waziri Mkuu Mizengo Pinda alishazitaka halmashauri zote za wilaya, kutenga maeneo hayo ili wamachinga waendeshe bishara zao bila bughudha.
ìIkiwezekana tutafukuzana na TAMISEMI ili kupata taarifa ya maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya wafanyabiashara hawa kabla bunge hili halijamalizika,î alisema
Alisema utekelezaji wa kutengeneza mazingira kuwezesha machinga hao kufanya kazi bila bughudha, unasimamiwa na TAMISEMI na kwamba, maeneo yaliyotengwa yatatangazwa ili kila mmoja ayatambue.
Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Janet Mbene alisema, mbali na kutenga maeneo kwa ajili ya wafanyabishara ndogo, wameandaa mkakati wa kutoa mafunzo kupitia SIDO.
Kupitia shirika hilo, alisema wafanyabishara hao wataweza kupatiwa mikopo yenye gharama nafuu kwa ajili ya kuendeleza biashara zao.
Awali, Martha Mlata (Viti Maalumu-CCM), alisema inasikitisha kuona wafanyabishara hao wanahangaika mitaani kwa kunyanyaswa na mgambo wakati wanachangia kwa kiasi kikubwa pato la taifa.
Alisema ni vyema serikali ikaja na mkakati madhubuti wa kuwasaidia wafanyabishara hao ili wafanye kazi katika mazingira mazuri na yanayokubalika.
ìHawa ni watu muhimu kwa uchumi wa nchi yetu, serikali inao wajibu wa kuwaandalia mazingira mazuri ili wafanye kazi kama wafanyabishara wengine kwani wanachangia kwa kiasi kikubwa katika uchumi wa nchi yetu,îalisema
Mwenyekiti wa Bunge, ambaye pia ni mbunge wa jimbo la Ilala, Azzan Zungu alisema, suala la wamachinga sio la kufumbia macho, badala yake linatakiwa kufanyiwa kazi kwa uhakika.
Zungu alisema hoja hiyo inaigusa miji yote, likiwemo jiji la Dar es Salaam, ambalo wamachinga wamekuwa wakinyanyaswa na mgambo wa jiji, licha ya kutokuwa na maeneo yaliyotengwa kwa ajili yao.
Alisema serikali itenge na kutangaza maeneo, ambayo wafanyabiashara hao wataendesha biashara zao bila kuumizwa.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru