Wednesday 14 May 2014

Kero mashine ya saratani kutatuliwa


NA SOPHIA ASHERY, DODOMA
SERIKALI imesema iutachukua hatua za haraka kutatua tatizo la mashine za kupimia saratani katika Hospitali ya Ocean Road zilizoharibika.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uratibu, Sera na Bunge), William Lukuvi, alisema serikali imepokea taarifa za kuharibika kwa mashine hizo takribani miezi miwili iliyopita.
Lukuvi aliyasema hayo jana alipokuwa akijibu hoja binafsi iliyowasilishwa bungeni na Esther Bulaya (Viti Maaalum-CCM), aliyetaka kufahamu hatua zinazochukuliwa baada ya kuharibika kwa mashine hizo ambazo zimesababisha usumbufu mkubwa.
Lukuvi, alisema licha ya hatua za haraka kuchukuliwa, serikali kupitia Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, itatoa ufafanuzi wa kina kuhusu suala hilo.
“Nimepokea taarifa kutoka kwa Mbunge wa Kigamboni, Dk. Faustine Ndungulile na sasa Esther, hivyo nataka kuwaambia kuwa waziri muhusika atalitolea ufafanuzi jambo hili,” alisema Lukuvi.
Esther, alisema maelfu ya wagonjwa wanaotegemea kupimwa kupitia mashine hizo hospitalini hapo, wamekuwa katika wakati mgumu huku wengine wakipoteza maisha baada ya kukosa huduma.
Alisema serikali inapaswa kulishughulikia suala hilo haraka ili kuokoa maisha ya wagonjwa ambao wapo katika hatari ya kupoteza maisha kwa kukosa huduma na hasa akina mama ambao wanasumbuliwa na saratani ya shingo ya uzazi.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru