Wednesday 28 May 2014

Mjamzito ajiua kwa sumu ya panya


Na  Latifa Ganzel, Morogoro
MAMA mjamzito aliyekuwa na mimba ya miezi tisa, Anjela Domiano (42), mkazi wa Nanenane katika Manispaa ya Morogoro, amefariki baada ya kunywa sumu ya panya.
Tukio hilo lilitokea juzi, saa 2.30 asubuhi, katika eneo la Kichangani katika Manispaa ya Morogoro.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Morogoro, Leonard Paul, alisema jana kuwa, marehemu
Angela alifia katika hospitali ya mkoa, ambako alipelekwa kwa ajili ya kupatiwa matibabu.
Alisema siku ya tukio, Angela alikutwa akiwa ameanguka huku akitapatapa katika eneo la Kichangani.
Alisema polisi walipata taarifa na kufika katika eneo la tukio na kumchukua mama huyo na kumfikisha katika hospitali hiyo, ambapo alifariki wakati akipatiwa matibabu.
“Wasamaria wema walipomwona mama huyo kaanguka chini, walitoa taarifa polisi na walipofika eneo la tukio, walimkuta akiwa anatapatapa na kuamua kumkimbiza hospitali ili kuokoa maisha yake,” alisema.
Alisema Angela alikutwa na sumu ya panya katika pochi yake na uchunguzi  wa awali umeonyesha kuwa, alifariki kutokana na kunywa sumu hiyo.
Kamanda huyo alisema hawakuweza kumhoji Anjela kutokana na hali yake kuwa mbaya  na wanaendelea na uchunguzi wa tukio hilo.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru