Sunday 25 May 2014

Vinara wa ‘mbwa mwitu’ wanaswa

NA William Shechambo

BAADA ya kikundi cha vijana wahalifu cha mbwa mwitu au panya road kufanya vurugu kwenye maeneo kadhaa ya jiji la Dar es Salaam mwishoni mwa wiki, Jeshi la Polisi Kanda Maalum limewakamata vijana sita ambao ni viongozi wa kundi hilo.

Vinara hao, Said Athuman (20), Joseph Mponela, Clement Peter (25) Roman Vitus (18), Mwinshehe Adam (37) na Daniel Peter (25) walikamatwa kutokana na msako mkali uliofanywa na jeshi hilo.

Katika mkutano wa dharura na waandishi wa habari uliofanyika jana ofisini kwake, Kamishna wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, alisema msako uliofanywa umezingatia maeneo yaliyokuwa yakisumbuliwa na kikundi hicho ambayo ni Kigogo, Magomeni, Tabata, Manzese na Mbagala.

Kova alisema ili kuhakikisha kikundi hicho na vingine vyenye tabia ya kufanya uhalifu na kusababisha uvunjifu wa amani jijni Dar es Salaam, vinadhibitiwa, askari wa kutosha wamejipanga kwenye maeneo hayo kwa ajili ya doria.

“Nimepanga askari wa kutosha kwenye maeneo hayo kwa ajili ya doria ili kudhibiti mlipuko wowote wa vitendo vya kihuni vyenye ishara ya uhalifu vinavyoleta hofu kwa wananchi,” alisema Kova.

Aliongeza kuwa Jeshi la Polisi limegundua mchezo unaofanywa na baadhi ya watu wa kutoa taarifa za uongo kwa umma kwa njia ya ujumbe wa simu za mkononi kuhusiana na kuvunjika kwa amani kwenye maeneo mbalimbali ya mkoa wa Dar es Salaam.

Alisema tabia hiyo ni mbaya na polisi linatoa onyo kali kwa sababu inasababisha hofu kwa wananchi huku kukiwa hakuna tukio lolote la uvunjifu wa amani kwenye maeneo husika.

“Kwa tekinolojia tuliyonayo, tuna uwezo wa kumtambua mtu au kundi la watu wanaosambaza ujumbe wa uongo ili kuwapa watu presha. Wenye tabia hizo waache mara moja kabla hatujawatia nguvuni,” alionya Kova.

Alisema upelelezi wao umebaini kuwa habari za uvunjivu wa amani uliofanywa na mbwa mwitu ambazo zilizotolewa wiki iliyopita, zilivumishwa kutokana na watu kufikiri kuwa kikundi hicho kitajitokeza hadharani kulipiza kisasi baada ya wenzao wawili kuuawa na wananchi Mei, 18 na 20, mwaka huu.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru