Wednesday 25 September 2013

Madereva kupimwa afya zao


Na Latifa Ganzel, Morogoro
SERIKALI imesisitiza mpango wa upimaji wa afya za madereva kwenda sambamba na ukaguzi wa magari ili kupunguza ajali za barabarani.
Alisema kwa kufanya hivyo, kutawahakikishia wananchi
usalama wao na mali zao.
Mkuu wa Wilaya, Saidi Amanzi, alisema hayo wakati wa ufunguzi wa Wiki ya Nenda kwa Usalama Barabara, ambayo inakwenda sambamba na upimaji wa afya kwa madereva katika maeneo ya Mikese mkoani hapa na Msoga, Pwani.
Kaulimbiu ya maadhimisho hayo kwa mwaka huu ni “Usalama barabarani inaanza kwangu, kwako na sisi sote.”
Amanzi alisema roho za abiria na mali ziko mikononi mwa madereva, hivyo hawana budi kutambua dhamana waliyonayo.
Kutokana na hilo, alikiagiza kikosi cha usalama barabarani kuhakikisha upimaji kama huo wa afya unakwenda sambamba na ukaguzi wa magari ili kupunguza ajali.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Ahmed Kipozi, aliwaasa madereva kuzingatia upimaji wa afya zao kutokana na dhamana waliyonayo ya kubeba watu, mali na mizigo yenye thamani kubwa.
Naye Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa, Boniface Mbao, alisema ni vyema madereva wakajenga tabia ya kupima afya zao kwa hiyari kwa manufaa yao.
Naye, Mwanasheria wa Kampuni ya Bia Tanzania (TBL), iliyodhamini shughuli hiyo, Steven Kilindo, aliahidi kushirikiana na kikosi hicho kuhakikisha ajali zinapungua kama si kumalizika kabisa.
Mpango huo pia unashirikisha Hospitali ya Mkoa wa Morogoro na Tungi Kibaha, ikiwa imelenga kuwafikia madereva 1,300 watakaopita barabara kuu za mikoa ya Morogoro na Pwani.
Ends.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru