Tuesday 3 September 2013

Mulugo ‘afunguka’ bungeni sekta ya elimu


SERIKALI imesema jitihada zinazofanyika za kuboresha sekta ya elimu, zinalengo la kuhakikisha shule zote nchini zinakuwa na mazingira rafiki ya kufundishia na kujifunzia.
Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philip Mulugo, alisema hayo jana bungeni mjini Dodoma, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Kilwa Kusini - CUF, Saidi Bungara, ambaye aliuliza matokeo mabaya ya kidato cha nne yanatokana na upungufu wa walimu.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri huyo alisema wazazi, walezi na jamii kwa ujumla, wanapaswa kuhakikisha suala la elimu linapewa kipaumbele katika ngazi zote.
Alisema elimu itawawezesha watoto kukabiliana na changamoto za elimu.
Mulugo, alisema ufaulu wa mwanafunzi unachangiwa pia na mambo mengi ambayo ni pamoja na jitihada za mwanafuni mwenyewe, ufuatiliaji na ushirikiano baina ya wazazi na walezi, pamoja na upatikanaji wa walimu, vitabu, maabara na mazingira mazuri ya kufundishia na kujifunza.
“Serikali inatekeleza mpango wa kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia katika shule zake za sekondari ili kuzifanya ziwe  rafiki.
“Mpango huo ni pamoja na ujengaji wa miundombinu ya maabara, vyumba vya madarasa na vyoo,’’alisema Mulugo.
Alisema serikali imejipanga vya kutosha na ndio maana katika mpango wa utekelezaji wa matokeo makubwa sasa, elimu imepewa kipaumbele kikubwa.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru