Tuesday 9 September 2014

3,000 wahitimu mafunzo ya polisi


Na Rodrick Makundi, Moshi
WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Haji Omar Kheir, atakuwa  mgeni rasmi katika sherehe za kufunga mafunzo ya awali ya askari polisi.
Mafunzo hayo yanayoendelea katika Chuo cha Taaluma ya Polisi Moshi (MPA) mjini hapa, yatafikia tamati keshokutwa ambapo wageni mbalimbali akiwemo Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali Ernest Mangu, watahudhuria.
Akizungumza na waandishi jana, Mkuu wa Chuo cha Taaluma ya Polisi Moshi, Matanga Mbushi, alisema wanafunzi wa uaskari 3,213 wanahitimu mafunzo hayo.
Kwa mujibu wa Mbushi, wanafunzi wa uaskari waliojiunga chuoni hapo walikuwa 3,509, ambapo 296 kati yao walishindwa kuhitimu mafunzo hayo kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo utovu wa nidhamu na kughushi vyeti.
Alisema wanafunzi 212 walifukuzwa kutokana na kubainika kuwa waligushi vyeti na wengine 84 wakifukuzwa kwa utovu wa nidhamu.
Idadi ya askari wanaohitimu mafunzo hayo inahusisha askari wa  uhamiaji waliojiunga na mafunzo chuoni hapo wapatao 43, ambapo wanaotarajiwa kuhitimu ni 41 wakiwemo wanaume 24 na wanawake 17.
Tofauti na miaka mingine, Mei 9, mwaka huu, jeshi la polisi lilitangaza kuwafukuza chuo askari 212, baada ya kuthibitika kughushi vyeti na wengine 25 waliachishwa mafunzo baada ya kubainika kuwa na matatizo ya kiafya na wengine utovu wa nidhamu.
Hatua hizo zilitokana na ushirikiano kati ya jeshi la polisi nchini na baraza la taifa la mitihani (NECTA), kufanya uamuzi wa kuhakiki vyeti vya wanafunzi wote 3,415 waliojiunga na mafunzo hayo Desemba mwaka 2013.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru