Tuesday 9 September 2014

Mkurugenzi apinga kurejesha fedha


Na Chibura Makorongo, Itilima
MKURUGENZI Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi, Abdallah Malela, amepinga agizo la kurejesha fedha za halmshauri mpya ya Itilima zilizotolewa na Hazina.
Pia anadaiwa kuwatimua ofisini kwake madiwani wa Itilima waliokwenda kudai fedha hizo.
Kauli hiyo ilitolewa katika baraza la madiwani wa halmashauri ya Itilima na Makamu Mwenyekiti wa Halmshauri, Khamis Mughata, ambaye alisema kamati yake ilishindwa kudai fedha hizo kutokana na mkurugenzi huyo kuwafukuza ofisi kwake.
Alibainisha kuwa kamati yake ilikuwa ikifuatilia mradi wa maji wa Lugulu-Zanzui ulioko ndani ya wilaya hiyo, ambapo walibaini ubovu wa miundombinu na matumizi mabaya ya fedha katika ununuzi wa vifaa.
Mughata alisema mradi huo ambao pesa zake ziko katika halmshauri ya Bariadi, ulikataliwa na mkurugenzi huyo kuukabidhi katika halmshauri yao, ikiwa pamoja na kukataa kutoa ushirikiano katika uchunguzi wa ubadhilifu huo.
Hata hivyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmshauri ya Itilima, Leornad Masele, alisema alishindwa kupata fedha wanazodai kutoka Bariadi kutokana na mkurugenzi huyo kugoma kukutana naye.
Awali, uongozi wa mkoa wa Simiyu, uliagiza wataalamu wa fedha wa kila halmshauri kukutana kwa ajili ya kuchunguza kiasi gani kinadaiwa, ambapo ilielezwa kamati hizo za wataalamu zilikuta na kupata takwimu sahihi za madeni hayo.
Alisema kwa maelekezo ya katibu tawala mkoa, wakurugenzi wote walitakiwa kukutana ili kumaliza hoja hiyo ya madeni, ambapo alieleza mkurugenzi mwenzake wa Bariadi amekataa kukutana naye bila kutoa sababu maalumu.
Katika kikao hicho, madiwani waliazimia kwenda kumshitaki mkurugenzi huyo kwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI) kwa kukaidi agizo la serikali kuu.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru