Tuesday 9 September 2014

Ajali yaua padri na wengine wanne

NA SOLOMON MWANSELE, MBEYA
WATU watano, akiwemo Padri wa Kanisa Katoliki, Paulo Mwanyalila, wamefariki dunia katika ajali mbili tofauti zilizotokea mkoani Mbeya.
Katika ajali hiyo iliyomwua Padri Mwanyanyila, gari lenye namba za usajili T241 BKZ aina ya Toyota Coaster, liligongana na gari liingine ambalo haijafahamika aina wala namba zake za usajili.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Ahmed Msangi,(pichani) alisema ajali hiyo ilitokea juzi saa moja jioni katika barabara ya Mbeya- Tukuyu, eneo la Garijembe, kata ya Utengule wilayani Mbeya.
Msangi alisema mbali

na Padri Mwanyanyila, wengine waliofariki dunia katika ajali hiyo ni Edina Jason (22), mtu moja aliyejulikana kwa jina la Mortina (30) na mwanamke mmoja ambaye hajajulikana jina.
“Katika ajali hii iliyoua watu wanne, pia ilisababisha watu watatu kujeruhiwa ambao ni Samwel Sanga (34), Mawazo Gasper na mtoto mwenye umri kati ya miaka miwili na mitatu, ambaye hakuweza kufahamika jina lake,” alisema.
Alisema chanzo cha ajali hiyo bado kinachunguzwa na kuwa miili ya marehemu imehifadhiwa katika Hospitali ya Rufani Mbeya na pia majeruhi wa ajali hiyo wamelazwa hospitalini hapo.
Msangi alisema madereva wa magari yote mawili walikimbia baada ya  ajali hiyo na msako mkali wa kuwatia mbaroni unaendelea ili waweze kufikishwa kwenye vyombo vya sheria kujibu tuhuma zinazowakabili.
Katika ajali ya pili, mtoto Grolia Revocatus (2), amekufa papo hapo baada ya kugongwa na gari katika barabara ya Mbeya- Iringa, eneo la Itewe wilayani Mbeya.
Msangi alisema ajali hiyo ilitokea juzi saa 1.30 usiku na kuwa dereva wa gari lililosababisha ajali hyo alikimbia baada ya kutokea kwa ajali hiyo na jitihada za kumtafuta zinaendelea.
Aliwataka madereva kuwa makini wanapotumia vyombo vya moto kwa kuzingatia sheria na alama za usalama barabarani ili kuepuka ajali.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru