Wednesday 3 September 2014

Korti yapokea simu 102 kama ushahidi


NA SYLVIA SEBASTIAN
MAHAKAMA ya Wilaya Ilala, imekubali kupokea simu 102, kama kielelezo cha shahidi Koplo Furahin ambaye alitoa ushahidi wa kesi ya wizi wa simu inayowakabili washitakiwa sita.
Pia imeamuru kwamba mwenye mali akabidhiwe simu zake kwa kuwa hazina pingamizi.
Washitakiwa hao katika kesi hiyo ni Idd Pawa, Hamada Mohammed, Haji Waziri, Yusuph Muhangwa, Hashimu Idd, Ally Omary na Mathias Ndunguru.
Washitakiwa hao walipanda kizimbani jana, mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi Juma Hassan kwa ajili ya kuendelea na shahidi wa nne upande wa Jamhuri.
Akitoa uamuzi huo, Hakimu Juma Hassan alisema mahakama imeamua kupokea kielezo hicho kama sehemu ya ushahidi wa upande wa Jamhuri.
Koplo Furahini alidai alikuchukua maelezo ya washitakiwa wanne na wote walikiri na kurudi mahabusu na Februari 4, mwaka huu, ambapo aliwapeleka kwa mlinzi wa amani katika Mahakama ya Mwanzo Ukonga.
Shahidi huyo alidai walikamata simu 102 na kila mmoja alikuwa na fungu lake la simu ambapo mshitakiwa Mohammed alikutwa na simu 15, Waziri (simu mbili), Mohangwa simu (10), Matihas (25) na mwingine alikutwa na simu 45, ambaye hayuko kwenye hati ya mashitaka.
Kesi imeahirishwa hadi Oktoba 9, mwaka huu, kuendelea na shahidi mwingine wa upande wa Jamhuri. Washitakiwa wako nje kwa dhamana.
Washitakiwa hao wanadaiwa Januari 27, mwaka huu,  katika Uwanja wa Ndege wa Kimatiafa wa Julius Nyerere,  Dar es Salaam, waliiba kasha  moja lenye simu 460 aina ya TECNO na Itel kutoka katika ndege ya Qatar iliyokuwa ikitoka China.
Inadaiwa simu hizo zina thamani ya sh. milioni 19.4 mali ya Sued Chemchem.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru