Friday 5 September 2014

JK: Nitaiacha nchi pazuri


Na Mwandishi Wetu
RAIS Jakaya Kikwete, amesema ataondoka madarakani akiwa ameiacha nchi mahali pazuri na kwamba, atakuwa na mengi ya kukumbukwa.
Amesema serikali yake imefanya mambo mengi kwa ajili ya Watanzania na kwamba, sekta karibu zote zimepiga hatua kubwa kimaendeleo.


Pia amewataka Watanzania kuombea mema mazungumzo baina yake na Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD), yenye lengo la kutafuta maridhiano kuhusu mchakato wa Katiba Mpya.
Ameeleza kuwa siku zote amekuwa akifungua milango kwa watu wanaotaka kumuona kwa ajili ya masuala mbalimbali ya kitaifa na angependa kuona mchakato wa Katiba Mpya ukikamilika kwa mafanikio.
Aliyasema hayo jana wakati akizungumza na wazee wa Mkoa wa Dodoma katika Chuo cha Mipango, ambapo alieleza masuala mbalimbali ya maendeleo na mikakati inayoendelea kufanywa na serikali.
“Nitaondoka madarakani nikiwa nimeiacha nchi mahali pazuri, ikiwa na mengi ya kukumbukwa na kuigwa.
“Tumejenga barabara nyingi za lami, miradi ya maji, umeme na elimu imeboreshwa kwa mafanikio makubwa. Tumepiga hatua kubwa na inastahili kuungwa mkono,” alisema Rais Kikwete.
Aliongeza kuwa pamoja na kupata mafanikio hayo, bado serikali imeendelea na jitihada zake katika kuboresha sekta mbalimbali na huduma za kijamii.
Alisema kuwa hivi karibuni atazindua miradi mingine mikubwa katika sekta ya elimu, ikiwa ni pamoja na Sera ya Elimu, ambayo tayari imekamilika.
Miradi ya maji
Alisema dhamira ya serikali ni kuhakikisha kuwa hakuna mtu atakayetembea kilomita nne bila ya kupata maji.
Rais Kikwete alisema hadi sasa asilimia 65 ya miradi ya maji imetekelezwa vijijini na asilimia 90 mijini.
Aliwataka wananchi kuhakikisha wanalinda vyanzo vya maji.
MIUNDOMBINU
Rais Kikwete alisema lengo la serikali ni kuunganisha barabara za lami mkoa kwa mkoa.
Alisema kwa mkoa wa Dodoma, sh. bilioni 44 zimetengwa kupeleka umeme vijijini.
Rais Kikwete alisema huduma za simu zimesambaa kwenye maeneo mengi hapa nchini na kwamba kazi iliyobaki ni ndogo.
ARDHI
Kiongozi mkuu huyo wa wananchi aliwataka viongozi wa mikoa na wilaya kuzingatia mipango ya matumizi ya ardhi.
Alisema mipango ya matumizi ya ardhi itaepusha migogoro mingi inayotokea hapa nchini.
Rais Kikwete alisema kuhusu migogoro ya ardhi iliyotokea Kiteto, Morogoro na Tanga, wanaangalia namna ya kuimaliza.
AFYA
Alisema mafanikio makubwa yamepatikana na kwamba amefurahishwa kuona wananchi wameshirikishwa kikamilifu katika sekta hiyo.
Rais Kikwete alisema wilaya za Kongwa, Bahi, Chamwino, Dodoma Mjini na Chemba hazina hospitali za wilaya, hivyo  aliwaagiza watenge maeneo na serikali itasaidia kujenga hospitali hizo.
Alisema mkoa wa Dodoma umevuka lengo kwa kina mama kujifungilia hospitali.
Rais Kikwete alisema maambukizi ya ukimwi yanapungua na kwamba ni vyema yafikie asilimia ziro.
EBOLA
Alisema taarifa zinaonyesha watu 3,500 wameambukizwa ugonjwa wa Ebola Afrika ya Kati.
Rais Kikwete alisema ugonjwa huo ni hatari na ambao ni mpya na kwamba hauna tiba wala kinga.
Alisema ugonjwa huo unabebwa na ndege kama sokwe, swala na popo na kwamba mtu anaweza kuambukizwa kwa kugusa damu, majimaji au maiti.
Rais Kikwete alisema dalili zake ni homa kali, kichwa kuuma pamoja na kutokwa damu sehemu zote zilizokuwa wazi.
Alisema tayari wameshaunda kikosi kazi kwa ajili ya kukabiliana na ugonjwa huo.
Mkutano na TCD
Kuhusu mkutano wake na wajumbe wa TCD, alisema Mwenyekiti wa kituo hicho, John Cheyo, alimuomba kukutana kwa ajili ya kuzungumzia masuala mbalimbali.
Alisema alikubali ombi hilo na Agosti 30, mwaka huu, walikutana na wajumbe wa kituo ambapo, masuala mbalimbali, ukiwemo mchakato wa Katiba Mpya na hatua ya kundi la Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) lilijitokeza.
Hata hivyo, alisema kuna baadhi ya mambo waliyokubaliana na kupeana majukumu juu ya namna ya kuyashughulikia na kuwa wanatarajia kukutana tena wiki ijayo.
“Tumekutana na kuzungumza, lakini tumepeana kazi za kufanya na tutakapokutana tena wiki ijayo, tutaona tumefikia wapi,” alisema Rais Kikwete.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru