Wednesday 3 September 2014

DAWASCO yawapoza wakazi Kidunda


NA  LATIFA GANZEL, MOROGORO
MAMLAKA ya Maji Safi na Taka Dar es Salaam (DAWASA), imewahakikishia wakazi wa Kidunda, wilayani Morogoro  kwamba inapitia upya  baadhi ya malalamiko juu ya fidia zao  katika mradi wa bwawa la Kidunda na kuyapatia ufumbuzi.
Hayo yalibainishwa jana na Mthamini wa Mali za DAWASA, Mhandisi  John Kwecha, alipzungumza na waandishi wa habari mjini hapa juu ya malalamiko hayo.
Alisema  baada ya kulipa fidia katika eneo la mradi wa bwawa la Kidunda, wamepokea malalamiko  ya wananchi 168 kati ya 1,239  ambao walilipwa fidia  ili kupisha ujenzi wa bwawa litakalosaidia upatikanaji wa maji katika mikoa ya Morogoro, Pwani na  Dar es Salaam.
‘’Tulianzisha dawati maalum kwa ajili ya kusikiliza malalamiko ya wananchi wakati wa ulipaji fidia hizo ili tuweze kushughulikia. Baadaye   tulipata malalamiko na tutayafanyia kazi kwa kufanya uhakiki upya ili kutenda haki,’’ alisema.
Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Said Amanzi, alisema uhakiki mali za wakazi hao, ulifanyika kwa kuwashirikisha wataalamu wa ardhi na viongozi wa vijiji kabla ya kuwapatia fomu zinaoonyesha mali zao.
‘’Katika jambo kama hili lazima kunatokea  upungufu, na kwamba suala la kulipa fidia lilianza Julai 23, mwaka huu, hadi sasa limemalizika. Tuache  dawati hilo lipitie kuona malalamiko hayo kama ni sahihi ili haki iweze kutendeka,’’ alisema Amanzi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro, Yona Maki. alisema ulipaji fidia kwa wananchi hao umekamilika kwa asilimia 90  na kwamba bado watu wachache ambao bado hawajakamilishiwa malipo yao kutokana na sababu maalumu, zikiwemo za taratibu za mirathi.
Alisema wananchi 1,218 kati ya 1,239 katika eneo la mradi wamelipwa na kwamba waliobakia ni wananchi 21, huku katika eneo la barabara inayopita katika mradi huo 1,318 wamelipwa bado 46 tu.
Hata hivyo, alisema ili kuwawezesha wananchi hao kuondoka katika eneo hilo la bwawa na kupisha mradi huo baada ya kulipwa fidia zao, halmashauri imetenga viwanja 1,000 kwa ajili ya wananchi hao.
Alisema tayari viwanja 300 vimeshapimwa  katika eneo la Bwira Juu kwa ajili ya wananchi hao na kwamba taratibu za upimaji viwanja vilivyobakia unaendelea.
Pia alisema wanatarajia kuchimba visima vitatu vya maji thamani y ash milioni 350 kuwawezesha wananchi hao kupata huduma ya maji safi.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru