Thursday 4 September 2014

MAUAJI YA MAHABUSU


Mazito yaibuka tena 

  • MOI yazuia jalada la marehemu, yataka malipo 
  • Familia, Polisi waendelea wavutana 
NA MWANDISHI WETU
MAITI ya mtuhumiwa aliyedaiwa kupigwa na kusababisha kifo chake akiwa mahabusu, imeshindwa kufanyiwa uchunguzi ili kutoa fursa kwa ndugu kuendelea na taratibu za maziko.
Liberatus Damian, alifariki dunia katika Hospitali ya Taifa Muhimbili baada ya kufikishwa kwa matibaabu akiwa hoi kwa kile kinachodaiwa kupigwa akiwa mahabusu katika Kituo cha Polisi Stakishari, Dar es Salaam.
Hata hivyo, jana ndugu na jamaa wa marehemu walifika hospitalini hapo kwa ajili ya mwili huo kufanyiwa uchunguzi, lakini ilishindikana baada ya uongozi wa Taasisi ya Mifupa na Mishipa yaFahamu ya Muhimbili (MOI), kuzuia jalada.
Jalada hilo lilizuiwa kutokana na taarifa kuwa marehemu anadaiwa zaidi ya sh. 260,000 za matibabu wakati alipofikishwa hospitalini hapo.
Kadhia hiyo imetokea ikiwa ni siku moja tangu Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, kuunda jopo la kuchunguza tukio hilo.
Habari zimedai, Damian alikuwa amehifadhiwa kituoni hapo na alifariki Agosti 31, mwaka huu, katika Hospitali ya Muhimbili alipokuwa akipatiwa matibabu.
Mwanasheria wa familia hiyo, Bagiliye Bahati, alisema jana walipanga kufanya uchunguzi wa mwili wa Daniel, lakini uongozi wa MOI ulizuia jalada.
Alisema walifika hospitalini hapo saa 3:00 na kukutana na jopo la wachunguzi hao wa polisi pamoja na wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora kwa ajili ya kuchunguza mwili.
Hata hivyo, uongozi wa MOI ulitaka kwanza kulipwa kwa deni hilo ndipo ukabidhi jalada hilo kwa hatua zinazofuata, ambapo polisi na familia walianza kurushiana mpira nani anapaswa kulipa.
Polisi walisema hawana fedha za kulipa deni hilo huku familia ikisema jeshi la polisi ndilo linapaswa kulipa kwa kuwa ndugu yao alipelekwa hospitali na polisi, ambao ndio waliosababisha matatizo yote.
Mwanasheria huyo alisema baada ya kutofikiwa kwa muafaka wa nani alipe, ilipofika saa 8:00 mchana, waliondoka na kukubaliana kukutana tena leo ili kutafuta ufumbuzi wa suala hilo.
Jitihada za kuutafuta uongozi wa MOI kwa ajili ya kulitolea ufafanuzi suala hilo zilishindikana baada ya wahusika kutokuwepo ofisini.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru