Wednesday 3 September 2014

NHC yakarabati majengo ya shule


NA SOLOMON MWANSELE, MBEYA
SHIRIKA la Nyumba la Taifa (NHC), limetumia sh. milioni 31.5 kukarabati majengo ya utawala na madarasa katika Shule ya Msingi Hassanga, iliyopo Uyole jijini Mbeya.
Hatua hiyo inatokana na ombi la Kamati ya Uongozi wa shule hiyo iliyowasilishwa na Ofisa Elimu wa wilaya kwa uongozi wa NHC mkoa wa Mbeya, mapema mwaka huu.
Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Abbas Kandoro,  akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi majengo hayo ambayo ni madarasa manne na jengo moja la utawala, alipongeza hatua ya NHC na kusema ni ya kipekee inayopaswa  kuwa mfano wa kuigwa.
Hafla hiyo ilihudhuriwa pia na  Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Nehemia Mchechu,  Meya wa Jiji la Mbeya, Athanas Kapunga, Kaimu Mkurugenzi wa jiji, Dk. Samuel Razalo na viongozi wengine.
“NHC hawalazimiki wala kulazimishwa kusaidia shule hii, lakini waliamua kutoa mamilioni ya shilingi kusaidia kuboresha miundombinu ili watoto wetu wasome kwa raha na amani.Hii ni ishara kuwa NHC inawajali Watanzania na lipo kwa ajili ya kuhudumia taifa,” alisema Kandoro.
Kwa upande wake, Mchechu alisema NHC imekuwa mstari wa mbele katika kusaidia huduma mbalimbali za kijamii.
Alisema katika jengo la utawala, ukarabati uliofanywa ulihusu ujenzi wa paa na  ujengaji upya wa ukuta.
Alisema majengo hayo sasa yana hadhi ya kisasa na NHC ina imani walimu na wanafunzi wataongeza ufanisi.
Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Neema Sanga, alisema shule ilianzishwa mwaka 1975 na ina wanafunzi 856 kati yao wasichana ni 438 na walimu waliopo kwa sasa ni 26.
“Shule imekuwa na mafanikio mazuri katika taaluma kwani, mwaka 2011 wanafunzi waliofanya mtihani walikuwa ni 79 na waliofaulu walikuwa ni 64, wakati kwa mwaka 2012, waliofanya mtihani walikuwa ni 123 na waliofaulu walikuwa ni 115,” alisema Neema.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru