Wednesday 3 September 2014

MBIO ZA URAIS 2015 Sitta awararua wapinzani wake

  • Awafananisha na wachekeshaji wa mfalme
  • Wasifu wake ukiaminiwa, atajitosa kuwania
  • Atuma salamu yuko imara, hatishiwi nyau
Na Happiness Mtweve, Dodoma 
MWENYEKITI wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta, ameibuka na kujibu mapigo dhidi ya watu wanaomkejeli na kumtolea lugha za matusi kuwa ni sawa na wachekeshaji wa mfalme.
Amesema yuko imara na kamwe hawezi kutishwa na kauli za watu wasio na maono na kwamba, ataongoza bunge hilo kwa kasi na viwango vile vile.
Akifungua kikao cha Bunge hilo baada ya wajumbe kurejea kutoka kwenye Kamati zilizogawanyika tangu Agosti 8, mwaka huu, Sitta alisema mambo mengi yalikuwa yakiendelea na alikuwa kimya.
Alisema kumekuwepo na matusi, kejeli nyingi na sasa kuna kesi iliyofunguliwa mahakamani dhidi yake na kwamba, kwa mtazamo wake haina uzito wowote.
Sitta, ambaye amekuwa akirushiwa makombora na baadhi ya wanasiasa wenye malengo binafsi, alisema pingamizi za kisheria zilizofunguliwa dhidi ya Bunge hilo hazina nia thabiti na kwamba nyuma yake kuna maslahi binafsi ya kusaka riziki.
“Nawasihi waheshimiwa wajumbe, msifadhaike na maneno ya kejeli tunayotupiwa hapa. Watu wanazungumzia posho na mambo mengine. Niko imara na kwa hulka yangu hizi kejeli na matusi ni kama vile maji katika mgongo wa bata kwani hawezi kulowana. 
“Kwa hiyo waendelee tu, pengine tunaanza kuwabaini na ni fursa nzuri na kuna rafiki yangu mmoja anaitwa Kubenea (Saed-Mhariri wa Kampuni ya Hali Halisi),” alisema Sitta na kuongeza: 
“Matukio yanayojitokeza dhidi yangu ni sawa na simulizi ya kuwepo wachekeshaji wa wafalme huko Ulaya kati ya karne ya 15 na 17.”
“Sasa wafalme wa Ulaya, waliajiri wachekeshaji kwa malengo mawili. Moja ni kumsikia mfalme kwa kila kitu, nyingine ni kuwasema wote ambao mfalme ni wabaya wake. Kwa hiyo kuna watu wa namna hii tunaanza kuwaona,” alisema.
Kuhusu dhana ya wasifu na nia yake ya kugombea urais katika uchaguzi mkuu ujao, Sitta alisema mpaka sasa hajatangaza nia, lakini kama watu wataonyesha kuvutiwa na wasifu wake, anaweza kujitosa kuwania nafasi hiyo.
Katika kile kinachoonekana kujibu shutuma za kisiasa kwa kiongozi wa CUF, Juma Haji Duni, kuhusiana na wasifu wake wa kugombea urais, Sitta alisema kiongozi huyo hana uwezo wa kumpima bali wenye uwezo wa kufanya hivyo ni wananchi.
“Nasema wanaochagua ni wananchi. Inawezekana mwakani Watanzania wakatamani mtu mzima aliyetulia na asiyeogopa wapuuzi, wakatamani hilo, mtu makini na mwadilifu. Basi kama itakuwa hivyo, wajue tupo na sisi wengine wa kuweza kufikiriwa katika nafasi hiyo nyeti,” alitamka Sitta na kuamsha shangwe.
Kuhusu utaratibu ulioanza kutumika bungeni jana, alisema wenyeviti wa kamati 12 waliwasilisha mapendekezo yaliyojadiliwa wakati wa kupitia Rasimu ya Katiba huku Kamati ya Uongozi ikipanga kila siku katika siku tano za kupokea taarifa za kamati.
Alifafanua kuwa, watapitia sura zilizoteuliwa ambazo ni Sura namba 2, 3, 4, 5, na kumaliza saa 12 jioni na kwamba, waliona ni vizuri kuwa na ulinganifu wa sura chache badala ya kamati moja kumaliza kusoma sura zote.
Aidha, wenyeviti hao walipewa muda wa dakika 20 kwa kusoma maoni ya walio wengi na dakika 10 kwa maoni ya walio wachache.
Sitta alisema wananchi wengi wameonyesha shauku ya kupeleka maoni yao katika Kamati ya Uongozi kinyume na ilivyokuwa ikitangazwa.
“Makundi mbalimbali ya wananchi waliosoma Rasimu, yamebaini ina mapungufu kama sisi kwenye kamati tulivyoona rasimu ina mapungufu na hili sio jambo la ajabu wala kupuuza kazi iliyofanywa na Tume hapana. Imefanya vizuri na tukumbuke ilipokea maoni kutoka kwa wananchi zaidi ya 334,000 na mabaraza zaidi ya 700, lakini walichokileta ni tafsiri yao kuhusu maoni hayo,”alisema Sitta.
Aliongeza kuwa chombo cha juu cha tume ni bunge hilo, ambalo ndilo lenye wajibu shahiri, kwa sababu baada ya kazi yake, halitarajiwi kutoa rasimu bali litatoa Katiba inayopendekezwa.
Alisema katika kipindi hiki, wameendelea na makundi na kujigamba kuwa yamekuwa msaada mkubwa kwa vile wametoa maoni na mengine yamekubalika katika kuboresha Katiba.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru